Meddie Kagere kuibukia kwa Alliance

Muktasari:

Ikicheza na Mbao FC kwenye dimba la CCM Kirumba, Simba ilimkosa straika wake tegemeo Meddie Kagere, ambaye alikuwa na kadi tatu za njano na sasa yuko tayari kukiwasha.

WAKATI Simba ikijiandaa na mchezo wake wa pili mfululizo jijini Mwanza, benchi la ufundi limesema haliwezi kuwadharau Alliance licha ya kwamba, hawajawahi kupata ushindi wala sare kwao.
Limesema kuwa kila mechi ni vita ya kusaka ushindi na kuendelea kujiweka nafasi nzuri ya kutetea ubingwa wao kwa mara ya tatu mfululizo.
Juzi Alhamisi Simba ilikutana na Mbao FC na kuondoka na ushindi wa mabao 2-1, kesho Jumapili itashuka dimbani kuvaana na Alliance FC uwanjani CCM Kirumba.
Vinara hao wa Ligi Kuu Bara wanakutana na wapinzani hao wakiwa na rekodi nzuri ya kushinda mechi zote nne walizokutana tangu Alliance wapande daraja msimu uliopita.
Meneja wa Simba, Rweyemamu amesema baada ya ushindi dhidi ya Mbao FC kwa sasa wanajipanga kwa Alliance ili kuondoka Mwanza wakiwa na alama sita mkononi.
Amesema licha ya rekodi kuwabeba, lakini wamejiweka kamili kukabiliana na upinzani kwani hakuna timu ndogo kwenye ligi na zote wanaziheshimu.
"Wachezaji wote tuliokuja nao wako fiti, hata Dilunga (Hassan) aliyeumia jana kwa sasa anaendelea vizuri, lakini na Kagere (Meddie) aliyekuwa na kadi tatu za njano amemaliza adhabu hivyo, ni kocha tu kama ataamua kumpa nafasi," amesema Rweyemamu.
Meneja huyo amefafanua kuwa kuhusu usajili wa wachezaji wapya ikiwa ni Shiza Kichuya na Luis Miquissone muda wowote wataonekana uwanjani baada ya vibali vyao (ITC) kukamilika.
"Ni kweli hao wote (Luis na Kichuya) ni wachezaji wetu ambao, tumesajili lakini kuna ishu za vibali ndio zinasubiriwa ila ndani ya siku moja au mbili mtawaona uwanjani,” alisema.