Matheo Anthony kumfunika Nchimbi Polisi

Muktasari:

Polisi Tanzania imeimarisha kikosi chake katika dirisha dogo kwa kuwana sa nyota watano akiwemo Pius Buswita na Matheo Antony.

MSHAMBILIAJI wa zamani wa Yanga, Matheo Antony ameahidi kuwa ataziba pengo la Ditram Nchimbi aliyetimkia Yanga kwenye dirisha dogo la usajili.
Matheo, ambaye amenaswa na Polisi Tanzania amesema kwamba, atafanya vitu vikubwa zaidi ili kuthibitishia mabosi zake wapya kuwa hawakukosea kumpa mkataba.
Mshambuliaji huyo amejiunga na Polisi Tanzania kwa mkataba wa mwaka mmoja baada ya Nchimbi kutimkia zake kwa mkataba wa miaka miwili.
Akizungumza na Mwanaspoti, Matheo alisema ameshaungana na timu yake mpya na muda wowote ataanza kukiwasha huku akifichua kwamba, kocha ndio ataamua kumtumia kwenye mchezo unaofuata ama la.
"Tayari nimeungana na wenzangu katika mazoezi, kikubwa nawaahidi mashabiki wa Polisi Tanzania kuwa, nimekuja hapa kupambana ili kusaidia timu yangu kuwa ya ushindani.
"Kuondoka kwa Nchimbi na kupewa nafasi hii ni heshima na ili kuthibitisha hilo nitafanya kazi kubwa na mashabiki watamsahau Nchimbi," alisema.