VITA BADO MBICHI: Sare ya Arsenal kicheko kwa Man City
Muktasari:
- Kwa matokeo hayo, yameifanya chama la Pep Guardiola, Man City kuchekelea na kuendelea kuwa katika mbio za ubingwa msimu huu.
LONDON, ENGLAND: SARE ya mabao 2-2 dhidi ya Wolves ugenini, imezidisha utamu katika mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu England, baada ya Arsenal kudondosha pointi mbili na kufanya pengo dhidi ya wapinzani wao wa karibu, Manchester City kubaki tano.
Kwa matokeo hayo, yameifanya chama la Pep Guardiola, Man City kuchekelea na kuendelea kuwa katika mbio za ubingwa msimu huu.
Arsenal ilihitaji ushindi ili kutanua wigo wa pointi dhidi ya wapinzania wao hao kwa kufikisha 60 na kufanya kuwa saba, lakini ilishindwa kufanya hivyo na sare hiyo kuifanya kufikisha 58ikiendelea kusalia kileleni.
Man City iko nafasi ya pili na pointi 53 na ina mechi moja mkononi dhidi ya Newcastle United itakayopigwa kesho Jumamosi na ushindi utaifanya kuisogelea Arsenal kwa tofauti ya pointi mbili.
Baada ya mchezo wa juzi usiku, Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta aliwakosoa vikali wachezaji wake baada ya sare hito na akikiri “hawakucheza kwa kiwango chao”.
Arsenal ilianza kuongoza kwa mabao mawili ya mapema ambayo yalifungwa na Bukayo Saka na Piero Hincapie kabla ya Wolves kuanza kusawazisha kwa bao la mbali la Hugo Bueno na bao la kujifunga la Riccardo Calafiori kuifanya mechi imalizike kwa sare hiyo.
Hata hivyo, Arteta aliyeonekana kuwa na hasira baada ya mechi, alisema kikosi chake hakikufikia kiwango kinachotakiwa.
“Ni vigumu sana kukubali. Kipindi cha pili hatukucheza kwa namna tulivyopaswa na kwa kiwango tunachohitaji kushinda mechi ya Ligi Kuu England. Ni bora tusizungumze sana kuhusu hilo kwa sasa, sote tumeumia. Lazima tukubali kufungwa kwa sababu tunastahili.
Ukiwa na huzuni na hasira ni rahisi kusema mambo yanayoweza kuidhuru timu. Kila mtu anataka kufanya vizuri. Lazima upitie nyakati ngumu. Leo dakika za mwisho tumelipa gharama. Tunapaswa kufanya mambo ya msingi vizuri zaidi kuliko tulivyofanya.”
Alipoulizwa kwa nini Arsenal hushindwa kushikilia bomba ipasavyo mara zote inapokuwa inaongoza Ligi Kuu England, Arteta alisema: "Leo lazima tukubali. Tunapaswa kujikosoa kwa sababu hatukufanya vizuri. Kwenye ligi, ukweli ni kwamba hatujawa katika kiwango chetu katika miezi ya karibuni. Ili uendelee kuwa juu lazima usimame imara."
Staa wa Arsenal, Saka naye alikosoa vikali wachezaji wenzake katika mahojiano yake ya baada ya mechi, akisema walionyesha kiwango kibovu kipindi cha pili baada ya Wolves kurejea mchezoni.
“Nimesikitishwa. Sina mengi ya kusema. Kulikuwa na tofauti kubwa kati ya jinsi tulivyocheza kipindi cha kwanza na cha pili. Tulishuka kiwango na tukaadhibiwa kwa hilo. Ni wakati wa kujitazama sisi wenyewe kama wachezaji."
MECHI TANO ZIJAZO ARSENAL
Tottenham (A) - February 22
Chelsea (H) - MachI 01
Brighton (A) - MachI 04
Everton (H) - MachI 15
Bournemouth (H) - April 11
MECHI TANO ZIJAZO MAN CITY
Newcastle (H) - February 21
Leeds United (A) - February 28
Nottingham Forest (H) - MachI 04
West Ham (A) - MachI 14
Crystal Palace (H) - TBC