Timu za EPL njia ngumu inazihusu

Muktasari:
- Msimu huu timu tatu kati ya nne za England zimefuzu moja kwa moja hatua ya 16 bora ambazo ni Liverpool, Arsenal na Aston Villa wakati Man City ikihitaji kucheza mechi ya mtoano kabla ya kutinga hatua hiyo.
MONACO, UFARANSA: KUELEKEA msimu ujao wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, timu sita za Ligi Kuu England zinatarajiwa kukabiliwa na droo ya kutisha ambapo kila timu itakutana na walau vigogo wawili wa Ulaya.
Msimu huu timu tatu kati ya nne za England zimefuzu moja kwa moja hatua ya 16 bora ambazo ni Liverpool, Arsenal na Aston Villa wakati Man City ikihitaji kucheza mechi ya mtoano kabla ya kutinga hatua hiyo.
Lakini timu sasa zinaweza kukumbana na changamoto zaidi msimu ujao, kulingana na matokeo ya droo inayotarajiwa kufanyika, Alhamisi ya Agosti 28, mwaka huu katika ukumbi wa Grimaldi Forum, Monaco. Timu tatu za kutoka nchi hiyo zimo kwenye Pot 01, ambazo ni Liverpool, Manchester City na Chelsea. Kila moja italazimika kucheza dhidi ya timu mbili kutoka Pot 01, na haziwezi kukutana na klabu kutoka nchi hiyo hiyo.
Washindani wakali zaidi kwenye Pot 01 ni Real Madrid, Barcelona, PSG, Chelsea, Borussia Dortmund, Bayern Munich na Inter Milan.
Kila timu katika hatua ya ligi italazimika kucheza dhidi ya timu mbili kutoka kila pot kwa hiyo yoyote kati ya Liverpool, City, Arsenal, Newcastle, Chelsea au Spurs inaweza kuishia kusafiri kwenda Bernabeu (Madrid) na Munich.
Pot ya pili pia ina timu hatari za Juventus na Atletico Madrid, pia kuna Bayer Leverkusen na Atalanta ambazo zimepata mafanikio makubwa hivi karibuni katika michuano ya kimataifa. Pot ya tatu inajumuisha mabingwa wapya wa Serie A Napoli, pamoja na Sporting Lisbon na PSV Eindhoven. Pot ya nne ambayo Newcastle imo pekee ya England, inaweza kuikutanisha na mabingwa wa Uturuki Galatasaray na wa Scotland Celtic, ingawa klabu hizo zinahitaji kupita hatua za kufuzu kabla ya kuingia ile ya ligi.