Mourinho atajwatajwa huko Nottingham Forest
Muktasari:
- Kocha huyo wa zamani wa Chelsea, Manchester United na Tottenham kwa sasa anainoa Fenerbahce ya Uturuki inayoshiriki ligi ya Turkish Super Lig.
LONDON, ENGLAND: KOCHA nguli, Jose Mourinho ameripotiwa huenda akarudi kwenye Ligi Kuu England kwa kishindo kwenda kuchukua mikoba huko Nottingham Forest endapo kama Nuno Espirito Santo atafutwa kazi.
Kocha huyo wa zamani wa Chelsea, Manchester United na Tottenham kwa sasa anainoa Fenerbahce ya Uturuki inayoshiriki ligi ya Turkish Super Lig.
The Special One, kama anavyofahamika na mashabiki, aliongoza klabu hiyo ya Uturuki kushika nafasi ya pili msimu uliopita na sasa amewekwa katika orodha ya makocha wanaowekwa kwenye mpango wa Forest.
Kwenye mchakato huo, Mourinho ameungana na kocha mwingine wa zamani wa Spurs, Ange Postecoglou.
Taarifa zilizopatikaka Ijumaa zilifichua nafasi ya Kocha Espirito Santo ipo kwenye mashaka makubwa baada ya kutibuana na mkurugenzi wa michezo wa klabu ya Forest, Edu.
Kumekuwa na wasiwasi kocha huyo Mreno, Espirito Santo anaweza kufunguliwa mlango wa kutokea ili makocha wengine kuja kupiga mzigo kwenye kikosi hicho cha Ligi Kuu England.
Kama hilo litatokea basi Mourinho anaonekana kuwa na nafasi kubwa ya kwenda kukipiga mzigo huko City Ground.