Mikel Arteta kuja na mbinu ya kivita
Muktasari:
- Kocha huyo kutoka Hispania tayari amewahi kutumia mbinu nyingine zisizo za kawaida, ikiwemo kuwaalika wezi ili kuwaibia wachezaji wake wanapokuwa wanakula chakula ili kuwafundisha umuhimu wa kuwa makini kila wakati.
LONDON, ENGLAND: KOCHA wa Arsenal, Mikel Arteta amefichua yupo katika mpango wa kushirikiana na marubani wa ndege za kivita wa jeshi la Uingereza ili kubuni njia mpya ya mawasiliano kwa wachezaji wake wanapokuwa uwanjani.
Kocha huyo kutoka Hispania tayari amewahi kutumia mbinu nyingine zisizo za kawaida, ikiwemo kuwaalika wezi ili kuwaibia wachezaji wake wanapokuwa wanakula chakula ili kuwafundisha umuhimu wa kuwa makini kila wakati.
Aidha, aliwahi pia kuwapigia wachezaji wake wimbo “You’ll Never Walk Alone” kupitia vipaza sauti wakati wa mazoezi, ili kuwatayarisha kisaikolojia kwa mazingira yenye makelele na presha kubwa ya uwanja wa Anfield kabla ya mechi yao dhidi ya Liverpool.
Sasa Arteta amekuja na ujanja mwingine. Akizungumza na rafiki yake na ambaye ni kocha mashuhuri wa mpira wa kikapu Steve Kerr, katika moja ya hafla ya Lead Better alisema:”Nataka kuwasiliana na marubani wa ndege jeshi la Uingereza ili kuiga wanavyowasiliana kwa sababu wale wanapowasiliana nina uhakika hawatumii maneno 20, huwa wanaweza kusema neno moja tu, kwa sababu ukiweka maelezo mengi unakuwa kwenye hatari ya kupoteza maisha, hivyo hiyo njia yao ya kuwasiliana itakuwa nzuri sana ikiwa tutaitumia uwanjani wakati wa mechi.”
Arteta aliongeza njia hiyo itapunguza kupoteza muda mwingi katika kuwasiliana kwa jambo moja, pia itawafanya wapinzani wao kutoelewana nini wanazungumza nini.
Msimu huu kocha huyu pia ameondoa sehemu ya juu ya mlango wa kuingilia uwanjani katika Uwanja wa Emirates ili kelele za mashabiki ziwafikie wachezaji pale wanapoingia.
Arteta pia amepeleka mbwa aina ya Labrador katika uwanja wa mazoezi ambaye hujumuika na wachezaji kila siku ya mazoezi.