Kisa umri, Ronaldo atupwa nje Saudia
Muktasari:
- Jorge ameviambia vyombo vya habari kuwa sababu kubwa ya kutomtumia mshambuliaji huyo wa Ureno kwenye mchezo wa leo ni kutaka kumpa muda wa kupumzika, kutokana na ushauri wa kitabibu aliopewa na jopo la madaktari wa klabu hiyo ya Saudi Arabia.
KOCHA wa Al-Nassr, Jorge Jesus, amesema Cristiano Ronaldo hatakuwa sehemu ya kikosi chake kitakachopambana na Al-Zawraa ya Iraq katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Asia leo Jumatano, Oktoba Mosi 2025.
Jorge ameviambia vyombo vya habari kuwa sababu kubwa ya kutomtumia mshambuliaji huyo wa Ureno kwenye mchezo wa leo ni kutaka kumpa muda wa kupumzika, kutokana na ushauri wa kitabibu aliopewa na jopo la madaktari wa klabu hiyo ya Saudi Arabia.
Amesema wanataka kumlinda Ronaldo, kwani ameshafikisha umri wa miaka 40 na ana hatari ya kuumia ikiwa atacheza mara kwa mara.
"Naona hiki ni kipindi bora cha kumpumzisha Cristiano Ronaldo. Kwa sasa ana umri wa miaka 40, na tunaogopa anaweza kuumia, ndiyo maana niliamua kumuondoa kwenye kikosi. Wachezaji wengine wana motisha kubwa ya kushinda na wanataka sana kufanya hivyo. Kwa hakika itakuwa mechi ngumu, lakini tuko tayari kushindana."
Jesus amezungumza na vyombo vya habari mwezi uliopita, akiwa na ishara kwamba wanazingatia ligi ya Saudia msimu huu na atamuweka benchi Ronaldo kwenye mashindano mengine.
"Nilikuwa nakusudia kumsaidia kuendelea kuwa na hali nzuri ya mwili na kujiandaa kwa mechi zijazo za ligi ya Saudi," amesema.
Al-Nassr ilimuajiri Jesus mwanzoni mwa msimu, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa klabu hiyo wa kusaka mataji msimu huu. Hata hivyo kocha huyo alikiri kwamba alijiunga na klabu hiyo kwa sababu ya Ronaldo.
"Bila mwaliko wake, si nisingekuwepo hapa. Motisha itakuwa kubwa. Nakuja kujaribu Al-Nassr, ambayo ni moja ya klabu bora nchini Saudi Arabia, kupata mataji. Ronaldo ni mchezaji ambaye ameshinda kila kitu katika klabu aliyocheza. Hajawahi kushinda katika Saudi Arabia bado. Nitaona kama naweza kumsaidia."
Cristiano Ronaldo amefunga mabao manne katika mechi nne za ligi msimu huu. Ana bao moja katika mechi mbili za Kombe la Super Saudia, lakini hajacheza katika Kombe la Mfalme na kwenye mashindano ya Ligi ya Mabingwa Asia (AFC Champions League) hadi sasa.