Jipange, ziko kambini zikiisubiri AFCON 2023 Ivory Coast

JANUARI ndio hii. Ile burudani ya mataifa 24 ya Afrika ndio hiyoo inakaribia. Ni kuanzia Januari 13 hadi Februari 11. Nani atataka kuikosa. Sidhani.
Miamba ya Africa inakutana kwenye fainali za Afcon Ivory Coast. Kila timu imeshatangaza kikosi kitakachosafiri kwenda kuiwakilisha nchi yake na Tanzania ikiwemo.
Zipo ambazo tayari zimeshaanza kambi za maandalizi na kuna zilizosafiri nchi nyingine na nyingine zimebaki nchini kwao.
Hii hapa ni ratiba ya timu shiriki na wapi zitaweka kambi zao kabla ya kusafiri kwenda Ivory Coast kwa ajili ya mashindano rasmi.
TANZANIA
Kambi - Misri
Taifa Stars kwa sasa ipo Jiji la Cairo, Misri ilikokita kambi. ikiwa huko, imepanga kucheza mechi ya kirafiki Januari 7, dhidi ya Misri kabla ya siku inayofuata kuanza safari ya Ivory Coast.
Kwa mujibu wa Ofisa habari wa TFF, Cliford Mario Ndimbo, baadhi ya wachezaji wachache walijiunga na kikosi kikiwa Misri ambao ni Himid Mao Mkami na Khelfin Hamdon.
Cameroon, Gambia, Zambia na Cape Verde
Kambi - Saudi Arabia
Timu nyingi zinaenda Mashariki ya Kati kutokana na hali ya hewa ya joto na inafanana na zitakapofanyika fainali hizo.
Saudi Arabia ni moja wapo na timu za taifa za Cameroon, Gambia, Zambia na Cape Verde zimeenda huko.
Cameroon na Gambia zipo kwenye kundi B na zitakutana Januari 23.
Cameroon ilisafiri kwenda Jijini Jeddad na kikosi chao cha wachezaji 23, Desemba, 27.
Gambia ilienda huko Desember 27 na inatarajiwa kumaliza kambi yao Januari 5 na itakwenda Morocco na itacheza mchezo wa kirafiki na timu hiyo Januari 7.
Zambia ilisafiri kwenda Saudi Arabia jana na imeweka kambi kwenye Jiji la Riyadh na itacheza mechi ya kirafiki January 07.
Burkina Faso, DR CONGO, Cape Verde, Nigeria, Angola, na Guinea
Kambi - United Arab Emirates
Burkina Faso ambayo ilimaliza nafasi ya nne kwenye mashindano ya mwaka jana, iliwasili Dubai Desemba 28 na inatarajiwa kuanzisha shindano dogo litakalozishirikisha Nigeria na DR Congo.
Baada ya kukaa kwa muda ndani ya Dubai vijana hawa wa Sebastien Desabre (Congo), watasafiri kwenda Abu Dhabi ambako itaungana na Cape Verde, kisha itaenda Tunisia Januari 10, kucheza dhidi ya Tunisia kwenye Jiji la Rades.
Kocha wa Guinea, Kaba Diawara alisema timu ilikusanyika kwenye Jiji la Conakry Desemba 28 na ilifanya sherehe za kuagwa na baada ya hapo wakasafiri hadi Abu Dhabi Desemba 31 na itaendelea kukaa kwenye jiji hilo hadi Januari 11 au 12, 2024, kabla ya kwenda Ivory Coast.
Nigeria pia itakuwepo Dubai kwa ajili ya maandalizi na itakutana na DR Congo na Burkina Faso na itacheza nazo mechi za kirafiki, pia huenda ikacheza dhidi ya Angola ambayo pia itakuwepo Dubai.
Ghana na Mozambique
Kambi - Afrika Kusini
Kabla ya mwaka huu kuanza tayari kikosi cha Ghana kilishawasili Afrika ya Kusini ambako wachezaji walisheherekea mwaka mpya wakiwa huko.
Ghana inaendelea na kambi yake ya siku 10 na inafanya mazoezi yasiyoruhusu kutazamwa na mashabiki na vyombo vya habari.
Itacheza mechi ya kirafiki dhidi ya Botswana Januari 8, kabla ya kusafiri kwenda Abidjan, Ivory Coast kuanza mashindano.
Msumbiji ambayo kwa sasa tayari imewasili Afrika Kusini itacheza mechi mbili za kirafiki kujiandaa na itaumana na Lesotho Januari 6, kisha Botswana Januari 8.
Algeria, Guinea Bissau, na Namibia
Kambi - Afrika ya Magharibi
Algeria imeamua kuweka kambi Togo kuanzia Januari 1 hadi 10 na wanakaa kwenye Jiji la Lome. Mabingwa hawa wa mwaka 2021 watacheza mechi ya kirafiki dhidi ya Togo Januari 5 kiha Burundi Januari 9.
Guinea Bissau itaweka kambi Mali na imecheza mechi ya kirafiki jana dhidi ya mwenyeji Mali na inatarajiwa kwenda Ivory Coast Januari 7.
Namibia itakuwa nchini Ghana.
Mauritania na Zambia
Kambi - Tunisia
Baada ya kumaliza harakati zao kule Abu Dhabi, Cape Verde itakuwa Tunisia na itacheza mechi moja ya kirafiki.
Mauritania itajichimbia maeneo ya Tabarka, mji ambao upo kaskazini, Magharibi mwa Tunisia.
Vijana hawa wa Amir Abdou watakuwa hapo hadi January 11 na watacheza mechi ya kirafiki dhidi ya mwenyeji Tunisia Januari 6.
HAWA WAMEBAKIA NYUMBANI
Morocco, Misri, Afrika Kusini, Guinea ya Ikweta, Tunisia, Mali, Senegal, na Ivory Coast, haya ni mataifa nane ambayo yamechagua kukaa kwenye nchi zao kwa ajili ya maandalizi ya mashindano haya.
Asilimia kubwa ya nchi hizi zina miundombinu mizuri ambayo inawawezesha wachezaji wao kujiandaa vyema kabla ya kwenda kupambania bendera za mataifa yao.