Hebu sikia hii kali ya Mascherano, Alonso

Muktasari:
- Mhispaniola, Alonso alithibitishwa kuwa kocha mpya wa Los Blancos akienda kurithi mikoba ya Carlo Ancelotti.
MADRID, HISPANIA: STAA wa zamani wa Liverpool, Javier Mascherano amesema anamwombea mabaya Xabi Alonso kwamba asifanikiwe kwenye kibarua chake mpya huko Real Madrid.
Mhispaniola, Alonso alithibitishwa kuwa kocha mpya wa Los Blancos akienda kurithi mikoba ya Carlo Ancelotti.
Alonso alitua Bernabeu akitokea Bayer Leverkusen, safari hii akipewa majukumu ya ukocha kwenye timu ambayo aliitumikia kama mchezaji kati ya 2009 na 2014.
Lakini, mmoja kati ya wachezaji wenzake wa zamani waliokuwa pamoja huko Liverpool amekuwa na maoni mbadala, akidai kwamba hawezi kumtakia heri kutokana na kwamba amekwenda kujiunga na timu ambayo yeye ni wapinzani wake kwa sababu aliwahi kukipiga Barcelona. Mascherano aliichezea Barcelona kwa miaka minane na kushinda mataji matano ya La Liga na mataji mengine kibao.
Aliponukuliwa na Marca, Mascherano alisema: “Bado sijaongea naye. Alikuwa mmoja wa wachezaji bora na nilicheza naye. Simtakii lenye heri kwa sababu yupo Real Madrid, lakini najua atakwenda kuwa kocha mzuri kwenye klabu.
“Alifanya kazi nzuri Bayer Leverkusen. Ni mtu safi pia, nilipata bahati kucheza naye kwa miaka mitatu.”
Wakati Mascherano akishindwa kumtakia heri Alonso huko Madrid, kocha huyo amefukuzia huduma ya kinda wa Kiargentina, Franco Mastantuono, ambaye atajiunga na Los Blancos akitokea River Plate.
Kinda huyo aliwahi kufundishwa na Mascherano kwenye kikosi cha vijana cha U-20 cha timu ya taifa ya Argentina na kwenye hilo, alisema: “Nilipata nafasi ya kumnoa kwenye timu ya vijana. Ni mchezaji mwenye kiwango bora kabisa na hakika ni wa kipekee. Anacheza soka la kupevuka.”