Havertz asubiri kwa hamu mziki wa Kante

MUNICH, UJERUMANI. KAI Havertz anasubiri kwa hamu kuuvaa mziki wa staa mwenzake wa Chelsea, N’Golo Kante wakati watakapokuwa wapinzani wiki ijayo kwenye mikikimikiki ya Euro 2020.

Havertz atakuwa kwenye kikosi cha Ujerumani, ambao watacheza mechi yao ya kwanza kwenye michuano ya Euro 2020 ndhidi ya chama la Kante, Ufaransa, Jumanne, Juni 15.

Kiungo Kante, 30, amezoeleka kucheza nyuma ya Havertz kwenye kikosi cha Chelsea, lakini mambo yatakuwa tofauti wakati mataifa yao yatakapokutana kwenye mechi za kusaka ubingwa wa Ulaya.

Havertz alisema: “Kante ni mchezaji mahiri. Nikiwa kama mshambuliaji, huwa nafurahi sana ninapomwona yupo uwanjani. Kwa sababu unaweza kupoteza mipira mara nyingi na yeye akairudisha kwenye himaya.

“Ana kazi, mpambanaji na siku zote yupo kwenye miguu yako. Ndio maana nasubiri kwa hamu kucheza dhidi yake kwenye michuano ya ubingwa wa Ulaya.”