Forest yajinasua kwenye hatari ya kushuka daraja EPL
Muktasari:
- Matokeo hayo yameifanya Forest kufikisha pointi 39, ikiwa na tofauti ya pointi nane dhidi ya Tottenham kabla ya mechi yao leo Jumamosi iliyo nafasi ya 18 na pointi sita dhidi ya West Ham iliyo nafasi ya 17.
LONDON, ENGLAND: USHINDI wa mabao 5-0 ambao iliupata Nottingham Forest jana Ijumaa ikiwa ugenini dhidi ya Sunderland katika mchezo wa Ligi Kuu England, umeisaidia timu hiyo kuwa mbali na hatari ya kushuka daraja huku kocha wa kikosi hicho, Vitor Pereira akieleza jambo.
Matokeo hayo yameifanya Forest kufikisha pointi 39, ikiwa na tofauti ya pointi nane dhidi ya Tottenham kabla ya mechi yao leo Jumamosi iliyo nafasi ya 18 na pointi sita dhidi ya West Ham iliyo nafasi ya 17.
Kwa sasa, kuna mjadala mkubwa nani atazifuata Wolves na Burnley huko Championship kati ya Tottenham na West Ham huku Forest na Leeds zikionekana kujiondoa katika hatari ya kushuka.
Kocha wa Forest, Vitor Pereira amesema pamoja na ushindi huo, wana kazi kubwa ya kufanya mbele yao ili kuwa salama zaidi.
“Hatuna pointi za kutosha bado. Tunahitaji kushinda zaidi na kudumisha nidhamu yetu,” amesema kocha huyo.
Hata hivyo, takwimu zinaonyesha historia inawapa matumaini Forest kwani hakuna timu iliyowahi kushuka daraja ikiwa na pointi 39 baada ya mechi 34 katika historia ya Ligi Kuu ya England. Kwa wastani, timu inayomaliza nafasi ya 18 huwa na takriban pointi 34 hadi 35.