Atletico yaiachia maumivu Barca Camp Nou
Muktasari:
- Wageni hao hawakuwa wamewahi kushinda katika Dimba la Camp Nou tangu mwaka 2006, lakini mabao katika kila kipindi kutoka kwa Julián Álvarez dakika ya 45 na Alexander Sørloth dakika ya 70 yaliwahakikishia ushindi katika mchezo wa kwanza wa robo fainali uliochezwa usiku wa Aprili 8, 2026.
Atlético Madrid wametanguliza mguu mmoja mbele kuelekea kufuzu nusu fainali ya UEFA Champions League baada ya kupata ushindi ugenini wa mabao 2-0 dhidi ya FC Barcelona iliyomaliza ikiwa pungufu ya mchezaji mmoja.
Wageni hao hawakuwa wamewahi kushinda katika Dimba la Camp Nou tangu mwaka 2006, lakini mabao katika kila kipindi kutoka kwa Julián Álvarez dakika ya 45 na Alexander Sørloth dakika ya 70 yaliwahakikishia ushindi katika mchezo wa kwanza wa robo fainali uliochezwa usiku wa Aprili 8, 2026.
Barcelona ilionekana kuwa bora kwa sehemu kubwa ya mchezo, lakini tukio la faulo dhidi ya Giuliano Simeone lililofanywa na Pau Cubarsí muda mfupi kabla ya mapumziko liliharibu kila kitu.
Awali beki huyo alionyeshwa kadi ya njano na mwamuzi István Kovács baada ya kumwangusha Simeone alipokuwa akielekea kufunga akiwa peke yake na kipa. Hata hivyo, uamuzi huo ulibadilishwa na kuwa kadi nyekundu baada ya mwamuzi huyo kushauriwa na VAR na kukagua tukio hilo upya kwenye skrini ya pembeni ya uwanja.
Álvarez aliizidishia Barcelona machungu kwa kupiga mpira wa adhabu uliokwenda moja kwa moja wavuni na kumnyima kipa nafasi ya kuokoa.
Licha ya kupungukiwa na mchezaji, Barcelona ilirejea vizuri na kutawala kipindi cha pili, huku Marcus Rashford akikaribia kusawazisha baada ya mpira wake wa adhabu kugonga mwamba wa juu wa lango.
Hata hivyo, badala ya Barcelona kusawazisha, ilijikuta ikiruhusu bao la pili, ambapo Sørloth alimalizia pasi ya chini kutoka kwa Matteo Ruggeri.
Matokeo hayo yanaiacha Barcelona na kazi kubwa ya kufanya itakaposafiri kwenda Madrid kwa ajili ya mchezo wa marudiano Jumanne ijayo.