Mondi, Zuchu imefika patamu....

ACHANA na shoo anazopiga nje ya nchi, huko jijini Paris Diamod Platnumz anaponda raha kinoma na mwanadada Zuhura Othman 'Zuchu'.
Nyota hawa wa muziki Tanzania (Bongo Flava) wameacha maswali kibao kwa mashabiki wao wanaojiuliza, Je, ni wapenzi au kiki?
Tangu alipoingia kwenye lebo ya Wasafi Classic Baby (WCB) mwaka 2020, Zuchu amekuwa na ukaribu na boss wake huyo na hakuna mahali ataenda bila ya yeye kutokuwepo.


APOTEZEA MAEX WAKE
Tangu ujio wa Zuchu, Mondi ni kama amekuwa naye bize kiasi cha kuacha au kutokuwa na mawasiliano na wanawake zake wa nyuma (EX) na kuongeza udaku wanatoka pamoja.
Dai amewahi kutoka na Wema Sepetu, Zarina Hassan (Zari), Hamisa Mobeto, Tanasha Dona na wengine na baadhi yao amezaa nao lakini kwa sasa hana time nao na anafanya mambo yake akiwa na Zuchu.


BATA KWA SANA
Wawili hao kwa sasa wameonekana jijini Paris, Ufaransa wakijiachia na kuponda raha na inasemekana Zuchu aliaamua kumfuata Bosi wake nchini humo. Diamond alitangulia kufika Paris na timu yake akiwemo manager wake, madansa, mpigapicha wake kwani alikuwa bado akiendelea na ziara yake ya kuitambulisha EP ya FOA Ulaya katika majiji ya Oberhausen, Ujerumani, Stockholm, Sweden kabla ya kwenda Paris na amekuwa akipatumia kama kituo chake anapokwenda kufanya shoo barani huko.
Pia walionekana wakifanya manunuzi katika maduka makubwa ya jijini na wamekuwa wakirusha video zao kwenye mitandao yao ya kijamii hasa Instagram.
Pia walijiachia kwenye migahawa ya chakula wakiwa katika pozi la mahaba, huku Zuchu akishindwa kujizuia na kuchezea saa ya Mondi kimahaba.
Zaidi ya yote waliobekana wakishikana na kutembea kwenye mitaa mbalimbali na kwenda sehemu za vivutio wakipigana picha.


WALIKOANZIA
Wawili hao walishaonekana pamoja sehemu mbalimbali ikiwamo kwenye uzinduzi wa Albamu ya Zuchu usiku uliojulikana kama 'Usiku wa Mahaba Ndi Ndi Ndi' kwenye Ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam kwenye Siku ya Wapendanao, Februari 14.
Kilichovutia ni waliwasili pamoja ukumbini hapo na gari la Mondi na kwenda kwenye 'red carpet' wakiwa wameshikana mikono.
Kwenye usiku huo, wengi walijua Mondi angemvisha pete Zuchu.


EP YAKOLEZA MAMBO
Wakati Mondi akipromoti EP yake ya FOA, alizua gumzo mitandaoni na aliwahi kukodi boti ya kifahari na kula maisha na patna wake huyo, wakicheza pamoja kimahaba Mondi alipokuwa akiimba wimbo wake wa Jeje.


LISTEN PARTY NAKO
Kujiachia pamoja sio mara moja moja, kwa sasa ni kama wameshazoea na walijiachia pia kwenye Listen Party ya Zuchu, nyumbani kwa mrembo huyo kwenye usiku wa utambulisho wa nyimbo zake mpya 'Fire' na 'Jaro'.


COLABO ZA MALAVIDAVI
Wawili hao wameshirikiana pia kwenye baadhi ya nyimbo kama 'Mtasubiri', 'Litawachoma' na 'Cheche' na zote zikiwa ni za kimahaba.


WAPINGA NI WAPENZI
Hata hivyo, wawili hao kwa nyakati tofauti wamekuwa wakikanusha udaku huo wakidai ni masuala ya kazi na si wapenzi.
Akihojiwa katika kipindi cha Salama Na kinachorushwa na Chaneli ya DStv, Maisha Magic Bongo aliulizwa ikiwa ni kweli yuko kwenye mahusiano na Diamond.
Zuchu alishikwa kigugumizi kutoa jibu moja kwa moja,  akisema hajui, mara hapana.
Kubwa kilichozua gumzo ni kuhusu kumpenda na alipoulizwa swali hilo, alipata pia kigugumizi kabla ya kujibu 'ndio napenda' ila hajui kama yuko kwenye mahusiano naye.
Hapa inaweza ikafichua ukweli wa mambo wawili hawa wapo kwenye mahusiano licha ya kuwa wakificha ukweli.