Yanga yamgombanisha kocha Mamelodi

Kocha Rhulani Mokwena

Muktasari:

  • Katika mechi ya mwisho kabla ya wiki ya mapumziko kwa ajili ya kupisha kalenda ya kimataifa wa Fifa, Sundowns ilicheza mchezo wa Kombe la Nedbank dhidi ya Maritzburg United katika  hatua ya 16 bora huku ikiwa haina wachezaji wake saba wa kikosi cha kwanza.

WAKATI mechi ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Yanga na Mamelodi Sundowns ikibakiza takriban siku tisa kuchezwa, huko Mamelodi kimenuka.

Ni hivi! Kocha mkuu wa timu ya taifa ya Afrika Kusini, Hugo Broos amesema amechukizwa na kitendo cha kocha wa Mamelodi Sundowns, Rhulani Mokwena kutangaza kwenye vyombo vya habari  kwamba wachezaji saba wa timu hiyo wanaumwa, hivyo hawatajiunga na timu ya taifa, badala ya watafuata taratibu zinazotakiwa.

Katika mechi ya mwisho kabla ya wiki ya mapumziko kwa ajili ya kupisha kalenda ya kimataifa wa Fifa, Sundowns ilicheza mchezo wa Kombe la Nedbank dhidi ya Maritzburg United katika  hatua ya 16 bora huku ikiwa haina wachezaji wake saba wa kikosi cha kwanza.

Mastaa hao ni pamoja na Ronwen Williams, Teboho Mokoena,  Themba Zwane ambao waliumia hivi karibuni wakiungana na Thapelo Maseko, Mothobi Mvala na Khuliso Mudau waliopo nje tangu waliporudi kutoka katika fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon) zilizopigwa Ivory Coast kuanzia Januari 13 hadi Februari 11, mwaka huu.

Licha ya kutokuwepo kwenye mechi hiyo Williams, Mokoena na Zwane walijumuishwa kwenye kikosi cha Afrika Kusini kinachotarajiwa kucheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya  Andorra na Algeria.

Baada ya kujumuishwa kwenye kikosi hicho Mokwena amesema Williams anatibiwa bega wakati Mokoena akisumbuliwa na tatizo la goti.

Siku kadhaa baada ya Mokwena kusema hivyo, Broos akiwa kwenye mkutano na waandishi wa habari amesema kocha huyo wa Mamelodi hajafikisha taarifa hizo kupitia njia sahihi, hivyo anachofahamu ni kwamba mastaa aliowaita wote ni wazima na anawataka kambini.

"Kama wachezaji kweli wameumia walitakiwa watuambie na sio kuzungumza kwenye vyombo vya habari. Tuna daktari na wao wanafahamu kwamba sisi tuna daktari na wana namba yake ya simu kwanini wasimpigie na kumpa hizo taarifa?" alihoji Broos na kuongeza:

"(Mokwena) hawakufanya hivyo ikiwa na maana kwamba wachezaji wote ni wazima. Samahani sana siwezi kufanya kazi kwa maneno yaliyosemwa na kocha Rhulani, labda mkurugenzi wa ufundi aniambie kwamba ni kweli wanaumwa.

"Tofauti na hivyo, wampe ripoti daktari wa timu (ya taifa) yeye ndio ataamua kwamba ni wagojwa kweli au la."

Taarifa zinaeleza kwamba Mamelodi haitaki kuwaachia mastaa hao kwa sababu wapo kwenye maandalizi ya mechi dhidi ya Yanga, hivyo wanahofia ikiwa watawaachia watapata muda mfupi wa kujiandaa na huenda wakapata majeraha zaidi.