Tanzania, Ivory Coast kusaini ' MOU ' sekta ya michezo

Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro leo Januari 26, 2024 amekutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Michezo wa Ivory Coast Mhe. Adjé silas na katika mazungumzo yao wamejadili juu ya kusaini makubaliano maalum ya ushirikiano (MOU) katika sekta ya michezo baina ya nchi hizo ili kuibua na kukuza vipaji.

Mhe. Ndumbaro ameipongeza nchi hiyo kwa maandalizi mazuri ya Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) yanayoendelea kwa kujenga miundombinu mizuri ikiwemo viwanja na barabara.

Amesema Tanzania inajifunza kwa Ivory Coast kwa kuwa itakuwa mwenyeji wa michuano hiyo kwa kushirikiana na Kenya na Uganda mwaka 2027.

Kikao hicho kimehudhuriwa pia na Kaimu Mkurugenzi wa Michezo kutoka Tanzania, Bw Ally Mayai na viongozi wengine wa Wizara ya Michezo wa Ivory Coast.