Siwa apangua kikosi Yanga

KUELEKEA mechi ya ufunguzi ya mashindano ya Kagame Cup kati ya Yanga ya Tanzania na Nyassa Big Bullets ya Malawi, Kocha wa makipa wa timu ya Yanga, Razak Siwa amepangua kikosi chake cha kwanza na kuwapa nafasi vijana chipukizi na wale waliokuwa wametolewa kwa mkopo na maingizo mapya.

Katika mechi hiyo inayotarajiwa kuanza saa 1:00 usiku kwenye uwanja wa Benjamin Mkapa, Siwa ameweka wazi kikosi cha Yanga kitakachoanza leo ambacho ni tofauti na kile kilichozoeleka kutumika kwenye mechi za Ligi Kuu Bara iliyomalizika mwezi Julai.

Katika eneo la golikipa leo Siwa amemuanzisha Ramadhan Kabwili, Mabeki ni Adeyum Saleh, Paulo Godfrey, Dickson Job na Abdallah Shaibu.

Eneo la kiungo na mawinga wataanza Chibada Kabago, Dickson Ambundo, Juma Mahadhi na Best Kahemela.

Waziri Junior na Ukonde ndio wataongoza safu ya ushambuliaji ya Yanga kwa leo huku katika benchi wakiwepo wachezaji kutoka timu ya vijana ya Yanga.

Ikumbukwe katika michuano hii kwa mwaka huu, Tanzania ikiwa wenyeji inawakilishwa na timu mbili tu za Yanga na Azam.