Siku tatu ngumu kwa TFF
BAADA ya mchujo wa awali kupita na mbivu na mbichi kujulikana sasa wagombea wa nafasi mbalimbali za uchaguzi wa TFF wanaingia katika siku tatu ngumu za mapingamizi.
Kuanzia leo Jumamosi hadi Jumatatu ni siku za wadau wa soka kuwasilisha mapingamizi kwa wagombea 20 wa nafasi ya urais na ujumbe wa Kamati ya utendaji ya TFF katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Agosti 7 mkoani Tanga. Baada ya siku tatu za uwasilishaji wa mapingamizi, Juni 22 hadi 24 itakuwa siku ya Kamati ya uchaguzi kusikiliza mapingamizi hayo kutoka kwa mlalamikaji na mlalamikiwa kabla ya Juni 25 hadi 27 wagombea kufanyiwa usaili.
Wagombea waliopitishwa kwenye mchujo wa awali ni Wallace Karia, Hawa Mniga na Evance Mgeusa ambao wanawania nafasi ya urais. Uchaguzi huo umekuwa na ushindani mkubwa huku ukivuta hisia za wadau wengi kutokana na mambo mbalimbali yaliyojiri.