Samatta ampigia kura Van Dijk, Ndayiragije kwa Messi
Muktasari:
Samatta atakutana na Van Dijk aliyempigia kura ya kuwa mchezaji bora wa dunia pamoja na Mane kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, Oktoba 23 ambapo KRC Genk itaanza kwa kuikaribisha Liverpool kabla ya kurudiana Anfield.
Dar es Salaam. Nahodha wa timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’, Mbwana Samatta alimpigia kura beki wa Liverpool, Van Dijk Virgil, Kaimu kocha mkuu wa Taifa Stars, Etienne Ndayiragije yeye alimpigia kura Lionel Messi katika tuzo za mchezaji bora wa dunia wa mwaka Fifa.
Cristiano Ronaldo wa Juventus na Lionel Messi wa FC Barcelona hawakuwa kati ya wachezaji watatu ambao Samatta aliwachanganua na kuona wanafaa kwa kuwapigia kura kuwa wachezaji bora kwa mwaka huu, 2019.
Hata hivyo, kura ya Samatta haikutosha kumfanya beki wa Liverpool kuwa mchezaji bora wa dunia, ambapo kwenye usiku wa jana kwenye jiji la Milan, alitangazwa Messi kutwaa tuzo hiyo kwa mara sita huku beki huyo wa Kiholanzi akishika nafasi ya pili.
Mbappe na Mane walipata kura za Samatta katika nafasi ya pili na tatu, hawakuweza kupenya kwa kuingia hata kwenye tatu bora ya wachezaji bora wa dunia.
Kaimu kocha mkuu wa Taifa Stars, Etienne Ndayiragije chaguo lake la kwanza lilikuwa Messi, akafuata Cristiano Ronaldo huku Mohamed Salah akiwa katika nafasi ya tatu.
Upande wa nahodha na kocha wa Uganda, Denis Onyango anayeichezea Mamelodi Sundowns F.C. , aliwachagua, Van Dijk, Salah na De Jong huku Abdallah Mubiru kwake ikiwa, Mbappé , Ronaldo na Messi
Kura ya Kenya, ilipigwa na mwandishi wa habari pekee, Toskin Robin kutoka ukanda wa Afrika Mashariki, ambayo alielekeza kwa Van Dijk, Ronaldo na Salah.