NBC yakabidhi zawadi kwa Maxime
Muktasari:
- Makabidhiano ya zawadi hizo yalifanyika muda mfupi kabla ya kuanza kwa mchezo baina ya KMC FC dhidi ya Kagera Sugar uliofanyika katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, mchezo ambao ulikamilika kwa timu ya KMC FC kuibuka na ushindi wa goli 2-0
Dar es Salaam. Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) ambaye ni mdhamini Mkuu wa Ligi Kuu ya Soka ya Tanzania Bara, NBC Premiere League jana ilikabidhi zawadi ya pesa na tuzo kwa kocha bora wa ligi hiyo kwa mwezi Februari, Mecky Maxime kutoka klabu Kagera Sugar.
Makabidhiano ya zawadi hizo yalifanyika muda mfupi kabla ya kuanza kwa mchezo baina ya KMC FC dhidi ya Kagera Sugar uliofanyika katika Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam, mchezo ambao ulikamilika kwa timu ya KMC FC kuibuka na ushindi wa goli 2-0
Katika tukio la makabidhiano ya zawadi hizo, ilishuhudiwa Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa wateja Benki ya NBC, Salama Mussa akikabidhi mfano wa hundi ya fedha yenye thamani ya Sh1 milioni sambamba na tuzo kwa kocha Maxime.
“Benki ya NBC kwa kiasi kikubwa tunaridhishwa na kasi ya ushindani inayoendelea kwenye ligi ya NBC. Zaidi pia na tunafurahishwa zaidi kuona mchezo huu unavyochochea ajira nyingine zisizo za moja kwa moja ikiwemo wafanyabiashara ndogo ndogo na kubwa wanaonufaika kupitia mauzo ya bidhaa mbalimbali zinazohususha mchezo huu zikiwemo jezi, huduma za vyakula na vinywaji kwa timu na mashabiki," alisema.
Salama alitoa wito kwa mashabiki wa mchezo huo kujitokeza kwa wingi kwenye viwanja mbalimbali ambapo michezo ya ligi hiyo inaendelea ili kufurahia na kuhamasisha timu zao ziweze kufanya vizuri zaidi kwa ushindani unaotakiwa.