Lwanga: Hawatuwezi!

Kiungo mkata umeme wa Simba, Thadeo Lwanga amesema mchezo wa leo walikuwa wanahitaji alama tatu na wamezipata mbele ya mabingwa mara 9 wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Al Ahly ya Misri.

Simba imeshinda bao 1-0 lililowekwa wavuni na Luis Miquissone dakika ya 30, Lwanga amesema waliwaheshimu Al Ahly ila uwanjani waliposhuka uwanjani ilikuwa ni mapambano ya kusaka ushindi.

"Ni timu nzuri kwenye ushambuliaji, tunawaheshimu nje ya uwanja ila ndani ni wachezaji 11 kwa 11 na leo wachezaji wote tulikuwa vizuri hatimaye tumeshinda," amesema Lwanga

Lwanga maarufu kama Injini amekuwa kwenye kiwango kizuri eneo la kati kwenye kikosi hicho katika mechi mbili za AS Vita ugenini na leo nyumbani.

Kiungo huyo raia wa Uganda ameeleza kuwa mbinu kubwa ilikuwa kucheza kwa nguvu kuhakikisha Al Ahly hawapati nafasi ya kucheza kutokana na ubora wa mpira wanaocheza.

Kocha wa wekundu hao wa Msimbazi, Didier Gomez amesema kwa namna walivyocheza wachezaji wake walistahili ushindi.