Hersi amtetea mtoto wa Manara
Msemaji wa Simba, Haji Manara ameonyesha kukerwa na mtoto wake wa kiume Hassan kurekodi video akitamba na jezi ya klabu ya Yanga anayoishabikia.
Wakati Msemaji wa Simba Haji Manara akionekana kukerwa na mtoto wake wa kiume kuvaa jezi ya Yanga kisha kutamba bosi wa GSM ambao ni wadhamini wa Yanga ameingilia kati ugomvi huo.
Manara kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram ameweka video ya kijana wake huyo wa kiume akiringia jezi ya klabu ya Yanga ambayo anaishabikia ambao ni watani wa jadi Simba ambayo baba yake anaishabikia na kuifanyia kazi.
Katika chapisho hilo Manara alienda mbali akisema adhabu ya kijana wake huyo ni kutomlipia ada ya shule.
"Nimefikiria kila hukumu kwa huyu mwanangu nimeona ni ndogo,okey atajilipia ada ya shule Januari hii na kwangu atahama," ameandika Manara ambaye ameoa mke hivi karibuni Nahida Abdallah ambaye naye ni shabiki wa Yanga.
Aidha Manara ameongeza akiandika"watu wamezaa watoto mimi nimejaliwa utopolo aisee'.
Baada ya kuandika hivyo Hersi ambaye ni Mhandisi na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Mashindano ya Yanga akajibu akimtaka Manara kutuma jina la shule ya Hassan na akaunti ya shule hiyo ili watume ada ya kijana huyo.
Aidha Hersi ameandika kwamba:"Tuachie mtoto wetu wewe tuma taarifa zifuatazo,jina la shule na akaunti namba,"ameandika Hersi huku akiongeza.
"Alafu mtafute akishakuwa Mhandisi,uje kula neema zake wakati huo rumba la mikia limekuzeesha.
Mbali na Hersi pia Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Yanga Arafat Haji naye ameandika kwamba:"Mtoto wetu (Hassan) hatutashindwa kumlipia ada lete 'invoice' tumlipie akasome Mwananchi huyu."