Hanspope: Simba isimkalie kimya Manara, yeye nani!

MJUMBE wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Zacharia Hanspope, amesema kitendo cha msemaji wa klabu hiyo, Haji Manara kusambaza sauti ikimtuhumu CEO, Barbara Gonzalez wa timu kuelekea mchezo wa Kombe la TFF ni kuihujumu timu.

Hanspope amefunguka hayo kama mwanachama na sio kiongozi wa timu hiyo huku akiweka wazi kuwa Simba ni timu kubwa haiwezi kumjubu.

Amesema Manara hakuwa na sababu ya kuzungumza mambo ya ndani mitandaoni alikuwa na nafasi ya kumtafuta kiongozi huyo au kwenda ngazi ya juu ili wayamalize kwa alichokifanya anakichukulia kama ni kuhujumu timu kuelekea mchezo wa ‘dabi’ unaotarajiwa kuchezwa Jumapili.

“Amekosa maadili kama hakuridhika na alichofanyiwa na CEO na yeye ni binadamu kama wengine anaweza kuwa anakosea lakini sio kwa namna aliyoitumia angeweza kwenda ngazi za juu apeleke malalamiko kwenye bodi,” amesema.

“Tukianza kuunganisha matukio tunaweza kusema anatumwa na hao watu anaowafanyia kazi maana mtu anapelekwa kwenye michango ya harusi analipwa Sh10 millioni eti michango ya harusi kumbe ni hongo kwa kazi fulani tunajua haya mambo yanatoke,” amesema Hanspope ambaye ameweka wazi kuwa yupo Simba kwaajili ya kuitengeneza timu hiyo iwe imara.


AFUNGUKA MSHAHARA WA HAJI

“Manara anamkataba wa Sh4 millioni amekataa kuusaini kwasababu anaogopa kujifunga na Simba kufuatia mambo mengine anayoyafanya nje ya klabu nasikitika ni kwanini amekuwa akizungumza kuwa analipwa lakisaba bila kutoa sababu,” amesema.

Amesema “Akitaka asaini mkataba wa milioni nne asifanye kazi sehemu nyingine sasa matokeo yake ndio hayo nani atamuamini anachokisema sasahivi anaweza akawa anatumwa na hao wanaomlipa aangalie sana haya mambo,”