Prime
Moloko hatoisahau Yanga, amtaja Nabi
ALIYEKUWA kiungo mshambuliaji wa Yanga, Mkongomani Jesus Ducapel Moloko amerejea tena nchini, ingawa safari hii amejiunga na kikosi cha Mbeya Kwanza cha mjini Tabora kinachoshiriki Ligi ya Championship kwa msimu huu.
Nyota huyo aliyewahi kuitumikia Yanga kuanzia Agosti 13, 2021 hadi Januari 28, 2024 akitokea AS Vita ya kwao DR Congo amejiunga na Mbeya Kwanza baada ya kuachana na AS Kigali ya Rwanda.
Moloko alijiunga na AS Kigali, Agosti 28, 2025, baada ya kuachana na ES Mostaganem ya Algeria ingawa hakudumu nayo baada ya kuondoka Januari 2026, huku akichezea timu mbalimbali zikiwemo za Diyala SC ya Iraq na Al Sadaqa Shahat SC ya Libya.
Baada ya kurejea nchini, Mwanaspoti limemtafuta nyota huyo na kupiga naye stori ambapo ameeleza mambo mengi ikiwemo maisha yake ndani ya Yanga na uhusiano wake na aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Nasreddine Nabi, sambamba na malengo yake.
KUMBUKUMBU NZURI YANGA
Moloko anasema miongoni mwa vitu ambavyo hatavisahau katika maisha yake ni kumbukumbu nzuri alizoziacha akiwa na kikosi cha Yanga, kutokana na ushirikiano mkubwa aliokuwa nao na wachezaji wenzake, tangu ametua kikosini humo hadi anaondoka.
“Kujiunga na Yanga ilikuwa jambo ambalo sitalisahau maishani mwangu, kwa sababu ni klabu yenye historia na mashabiki wa ajabu, nilipofika lengo langu lilikuwa rahisi, kwanza, kufanya kazi kwa bidii na kujitoa kwa ajili ya timu,” anasema.
Nyota huyo, anasema jambo lililompa urahisi wa kuzoea mazingira kwa muda mfupi ni kutokana na mtindo wa uchezaji ambao unategemea nidhamu, nguvu na ushirikiano na wachezaji wenzake ambao ulizidi kuimarika siku baada ya siku kikosini humo.
“Kuna mechi zinazonijia katika kumbukumbu zangu, ila, nyakati bora zaidi zinabakia zile ambazo tulishinda tukiwa mbele ya mashabiki zetu, kwa sababu mazingira uwanjani yalikuwa ya ajabu, kutokana na hamasa zao kwetu wachezaji,” anasema.
NABI NDIYE KOCHA BORA
Moloko anasema licha ya kufundishwa na makocha wengi wazuri, lakini kwake aliyekuwa kocha wa Yanga, Nasreddine Nabi ndiye atakayebaki katika kumbukumbu nzuri katika maisha yake kutokana na jinsi alivyokuwa anajua kuishi na wachezaji.
“Binafsi nilifurahia sana kufanya kazi na Nabi, ni kocha anayejua jinsi ya kuwahamasisha wachezaji na anajenga ile hali ya kujiamini katika timu, pia, nilijifunza mengi, hususani mbinu na mawazo mapya, jambo lililonikuza maishani,” anasema.
Nyota huyo anasema mbali na hilo, ila Nabi alimfanya kuamini kuna wakati mzuri uko mbeleni hata kama kuna changamoto za aina yoyote, jambo lililomsaidia kwa kiasi kikubwa kufanya kazi kwa bidii na kupigania malengo ya timu na yake kiujumla.
“Nabi alichukua jukumu muhimu sana la ukuaji wangu Yanga, ni kocha anayejua muundo wa timu jinsi ya kucheza kutokana na mpinzani tunayekutana naye, lakini yote hayo aliyafanya kwa kutegemea pia nidhamu, nguvu na ushirikiano kwa kila mmoja.”
MASHABIKI YANGA USIPIME
Moloko anasema katika mambo asiyoyasahau ni jinsi mashabiki wa Yanga wanavyoipenda na kuifuatilia timu yao popote pale inapokwenda kucheza, jambo ambalo lilikuwa linawapa hamasa wachezaji ya kuzidi kupambana uwanjani kwenye kila mechi.
“Mashabiki wa Yanga ni wa ajabu sana, shauku yao kwa klabu ni kubwa na inawapa wachezaji nguvu nyingi uwanjani, lakini shinikizo la kushinda ni la kawaida na ndio maana timu imekuwa na mafanikio makubwa kutokana na msukumo unaopatikana.”
Nyota huyo anasema mbali na mashabiki ambao ndio chachu ya wao kufanya vizuri na kuisaidia timu kutwaa mataji mbalimbali nchini, ila jambo lingine lililomsaidia kumudu presha hiyo ni wachezaji wenzake, ambao walimpa ushirikiano tangu mwanzo.
“Wachezaji wenye uzoefu walinisaidia sana, walinifundisha jinsi ya kushughulikia mechi kubwa na jinsi ya kubaki makini katika nyakati muhimu, ushindi huleta furaha na kujiamini, lakini, kushindwa hutusukuma kufanya kazi kwa bidii zaidi.”
LIGI YA TANZANIA NOMA
Licha ya nyota huyo kucheza nchi nyingi katika karia yake ya soka, ila, anasema miongoni mwa Ligi bora ni ya Tanzania, kutokana na jinsi mashabiki wanavyopenda timu wanazoshabikia, kitu ambacho kwa wengine ni ngumu pia kukiona kila mechi.
“Ili Ligi ionekane imepiga hatua kuna vitu vingi sana vinachangia, ambapo kwanza ni uwepo wa wachezaji wakubwa kutokea mataifa mbalimbali ambao tayari Tanzania tunazidi kujionea, ila, msukumo wa mashabiki pia unachangia kwa kiasi kikubwa.”
Moloko anasema kwa mchezaji yeyote anayetaka kufanikiwa na kufikia malengo yake katika Ligi ya Tanzania iwe ni mzawa au wa nje ya nchi ni lazima awe na kipaji, akili ya kufikiria mambo kwa haraka na jinsi ya kuyachuja na kuzingatia nidhamu.
NJIA NYEUPE YANGA
Anasema ikiwa itatokea Yanga ikamuhitaji tena kwa ajili ya kuichezea timu hiyo kwa sasa yupo tayari kutokana na jinsi ambavyo anaipenda, ingawa msimu huu malengo yake ni kuisaidia Mbeya Kwanza, aliyojiunga nayo kwa mkataba wa miezi sita.
“Kuichezea Yanga katika Ligi hii ni jukumu kubwa lakini pia ni chanzo kikubwa cha fahari, ikiwa itatokea fursa ya kurudi ningefurahi, kwa sababu klabu hiyo itabaki maalumu maishani mwangu na kamwe sitaweza kusahau kwa nyakati zote,” anasema.
YANGA INAVYOIPIGA BAO SIMBA
Nyota huyo anasema siri kubwa ya Yanga kufanya vizuri kwa misimu ya hivi karibuni ni kutokana na ushirikiano mzuri wa mawazo ya ushindi kutoka kwa uongozi na mashabiki, tofauti na ilivyokuwa kwa wapinzani wao wakubwa nchini timu ya Simba.
“Ili timu ionekane inafanya vizuri kuna vitu vingi vinachangia kufikia malengo hayo, kwa mfano Yanga viongozi wote na mashabiki wana shauku ya kuona inabeba makombe mbalimbali, hiyo inasababisha tu wachezaji wazidi kupambana kila mechi.”
MAISHA NJE YA YANGA
Licha ya kuipenda Yanga, ila nyota huyo anasema aliona ni muda mzuri wa kuondoka kwa ajili ya kwenda kujifunza mazingira tofauti na ya Tanzania, kitu kilichomsaidia kuongeza taaluma yake na kuboresha kiwango chake kutoka pia mataifa mengine.
“Kucheza katika nchi tofauti kuliniruhusu kujifunza mambo mengi, kuhusu mpira wa miguu na tamaduni za maeneo mbalimbali na jinsi wengine wanavyoishi, kwa mfano Ligi za Algeria na Iraq, zina mahitaji makubwa ya kimwili na kimbinu,” anasema.
Nyota huyo anasema licha ya kuondoka kwake, ila mashabiki wa Yanga wataendelea kumkumbuka kutokana na upiganaji wake kwa ajili ya timu muda wote aliocheza ndani ya kikosi hicho, kwani tofauti na mataji, ila alipata uzoefu na ukomavu mkubwa.
“Maisha ya mchezaji wa mpira wa miguu nje ya nchi yanahitaji sana kuzoea na kudumisha nidhamu kuanzia ndani na nje ya uwanja, Kila Ligi ina changamoto zake, kasi, shinikizo na utamaduni mpya, ambapo usipokuwa makini hutaweza kuvumilia.”
KILICHOMRUDISHA BONGO
Moloko anasema sababu kubwa iliyomrudisha tena Tanzania ni kutokana na fursa mbalimbali alizozipata, huku akiwa na hamu ya kuendelea kucheza na kutoa uzoefu wake, baada ya uongozi wa Mbeya Kwanza kumfuata na kuhitaji huduma yake msimu huu.
“Malengo ya timu ni kucheza Ligi Kuu Bara msimu ujao, sasa baada ya mabosi wa Mbeya Kwanza kunihitaji nilivutiwa zaidi na mradi wao kiujumla, hivyo, ninataka kuleta uzoefu wangu na kusaidia kukidhi matarajio ya mashabiki,” anasema Moloko.
Nyota huyo anasema kurudi kwake nchini na kujiunga na Mbeya Kwanza inayoshiriki Ligi ya Championship msimu huu sio jambo la ajabu kwa sababu ya wasifu wake, isipokuwa ni fursa ya kuongeza uzoefu na kupigania malengo ya timu hiyo kwa ujumla.