Mtanzania achapwa kwa TKO Nigeria akiwania ubingwa wa dunia

Muktasari:

Mkalekwa ameendelea kuweka rekodi ya kuchapwa mfululizo na mabondia kutoka nje ya nchi ambapo pambano la Nigeria ni la nne kuchapwa, wengine waliomchapa ni Tewa Kiram, Eric Kapia, Andreas Valavanis na Anthony Jarmann.

Salehe Mkalekwa ameshindwa kuvunja rekodi ya  Rilliwan Ayodele Babatunde wa Nigeria ya kutopigwa kwa miaka mitano mfululizo katika pambano lao la kuwania ubingwa wa dunia wa WBF usiku wa kuamkia jana.

Mkalekwa ameruhusu kipigo cha Technical Knock Out (TKO) katika pambano hilo la raundi 12 la uzani wa welter lililopigwa nchini Nigeria.

Babatunde ameendeleza rekodi ya kutopigwa tangu mwaka 2016 alipoingia rasmi kwenye ngumi za kulipwa ambaye amecheshapigana mapambano 13.

Mtanzania alikubali kipigo cha TKO kwenye uwanja wa Teslim Balogun, mjini Lagos.

Katibu Mkuu wa wakala wa ngumi za kulipwa Tanzania (PST), Anthony Rutha amesema Mtanzania huyo alizidiwa mbinu na mpinzani wake aliyekua akicheza nyumbani.

Licha ya Mkalekwa mwenye rekodi ya kucheza mapambano 25 na kushinda 15 (4 kwa KO) na kupigwa mara tisa (4 kwa KO) alipanda ulingoni akibebwa na uzoefu wa ndondi kwa miaka 14 alishindwa kutamba mbele ya mwenyeji huyo aliyeingia ulingoni akionyesha nia ya kutaka kumaliza pambano hilo mapema.

"Mkalekwa alizidiwa tu mbinu na mpinzani wake ambaye alionekana yuko fiti muda wote," amesema Rutha.

Kipigo hicho uenda kitampromosha kwenye renki  Mkalekwa ambaye ni bondia namba mbili kati ya 31 nchini na wa 423 kati 1,962 duniani kwenye uzani wa welter.