Marioo ang’ara wateule tuzo za Afrima, atajwa vipengele sita

Msanii Omar Mwanga maarufu kwa jina la Marioo ameng’ara katika majina ya wateule watakaoshindanishwa katika Tuzo za All Africa Music Awards(Afrima) mwaka huu 2022.
Majina ya wateule hayo yaliwekwa hadharani jana Septemba 14, 2022 katika mtandao wa Afrima huku Mario akionekana kujitokeza katika vipengele sita  kupitia wimbo wake wa Mi Amor alioimba kwa kumshirikisha msanii Jovial kutoka nchini Kenya.
Wimbo huo aliouachia Februari mwaka huu, mapaka sasa umeshatazamwa mara milioni 18 na kufanya kuwa wimbo wake uliotazamwa zaidi tangu aingine kwenye muziki.
Vipengele ambavyo Marioo ametajwa ni pamoja na msanii bora wa kiume Afrika Mashariki, ambapo atachuana na wasanii wengine kutoka Tanzania akiwemo Diamond Platnumz, Rayvanny na Mbosso.
Vipengele vingine alivyotajwa msanii huyo ambaye kwa sasa anafanya vizuri na wimbo wake wa Dear X, ni wimbo bora wa kushirikiana, wimbo bora wa mwaka, wimbo bora wa Rnb na Soul na mtayarishaji bora.
Ukiacha Mario wengine wapya waliojitokeza katika tuzo hizo ni  Frida Amani kupitia wimbo wake wa Tanzania Tanzania, na Nay wa Mitego kupitia wimbo wake wa Rais wa Kitaa ambaye anashindanishwa katika kipengele cha Rapa bora na wimbo bora wa Rap.
Hata hivyo kwa upande wa msanii Diamond Platnumz ameendelea kuonyesha makali yake katika tuzo hizo, ambapo ameingia katika vipengele vinne kupitia wimbo wa Mtasubiri ikiwemo msanii bora wa kiume,msanii wa mwaka ,albamu ya mwaka kupitia albamu yake ya ‘First of All’ aliyoiachia mapema mwaka huu.
Wasani wengine waliotajwa kwenye tuzo hizo wapo Pia yupo Rosa Ree, Navy Kenzo, Nandy na Zuchu.