Billnass, Young Lunya kumfuata Whozu

Muktasari:

Billnass na Young Lunya ni miongoni mwa wasanii wa muziki wa rap ambao wanafanya vizuri kwa sasa hapa nchini.

RAIS wa lebo ya muziki (Too Much Money), Fred Vunjabei amesema wapo kwenye mazungumzo na wasanii, Young Lunya na Bilnass ili kufanya nao kazi kwenye lebo bayo.

Fred ambaye pia ni mmiliki wa maduka ya Vunja Bei,  akizungumza leo Jumatano Septemba 30, 2020 amesema wanataka kuifanya lebo yao kuwa miongoni mwa lebo kubwa ya wasanii ndani na nje ya nchi.

"Mimi na Billnas ni marafiki lakini nataka tufanye wote kazi, hilo pia lipo kwa Young Lunya na msanii mwingine Odong Odwaa ambaye anasifika katika muziki wa kuchana (mitindo huru)" amesema Fred.

Akizungumzia kuhusu changamoto ambazo zipo kwenye usimamizi wa wasanii, amesema ni kuwekeza pesa nyingi huku ukiwa hujui ni lini unaweza kurejesha pesa yako.

"Huku unaweka pesa lakini haujui ni lini utairejesha, mfano kwa sasa Whozu ni msanii mkubwa lakini na yeye tulianzia huko huko, lakini siku hizi anasaini mikataba mingi, kikubwa kwenye muziki ni uvumilivu tu" amesema Fred ambaye pia anakuwa anawavalisha wasanii mbalimbali kupitia maduka yake.

Fred ameongeza kwa kusema anataka lebo yake kuwa na wasanii 30 na baada ya hapo ataanza kufanya matamasha mbalimbali kama zilivyo lebo zingine.

Katika lebo ya Too Much Money mpaka sasa inamsimamia msanii Whozu ambaye anatamba na ngoma ya Aah Wapi, nyingine ni Roboti na Follow Unfollow.