Mr Blue ampa saluti Maua Sama

Muktasari:

Mau Sama ametaja kama mwanamuziki wa kike ambaye akikaza buti anaweza akatikisa ulimwenguni kutokana na aina ya muziki anaoufanya.

MSANII wa Bongo fleva,Herry Sameer 'Mr Blue' amesema kama kuna wasanii wa kike ambao wamepiga kazi mwaka huu basi ni Maua Sama.

Mr Blue amesema Maua Sama anafanya muziki wake kisasa, jambo analoamini baada ya miaka kadha atajulikana ulimwenguni.

Amesema ameutazama mwanzo wa Maua Sama ameuona una misingi ya muziki wa kisasa na kubwa zaidi ni namna anavyotunga nyimbo zinazodumu kwa muda mrefu masikioni mwa mashabiki.

"Maua Sama ni mwanamuziki mzuri kwa upande wa wanawake na nimeona ana vitu ambavyo vinatakiwa kwenye muziki wa kisasa, ninachomshauri akaze buti ili afike pale tunapotarajia kumuona,"alisema.

Mbali na hilo alisema anaamini msanii huyo anaongozwa na watu makini wenye jicho la kujua nini kinatakiwa kwenye gemu la muziki wa sasa.

"Naamini Maua Sama ana watu ambao ndio washauri wa muziki wake, wapo vizuri kwa sababu kadri anavyofanya kazi zake unamuona ni mtu anayeingia anga kubwa hajatazama hapa nyumbani tu,"amesema.