Mwambusi afurahi kuhairishwa kwa mechi ya Yanga

Muktasari:

Mwambusi anakinoa kikosi hicho kwa mwaka mwingine baada ya kuachana nacho na kutimkia katika klabu ya Yanga baadaye Azam FC na sasa amerudi kwa msimu mwingine.

Dar es Salaam.Kocha Mkuu wa Mbeya City, Juma Mwambusi amesema amelipokea kwa furaha suala la kuhairishwa kwa mchezo wake dhidi ya Yanga na kuweka wazi kuwa anahitaji mechi kumi ili kupata kikosi cha kwanza.

Yanga na Mbeya City zilipangwa kukutana Agosti 18 mwaka huu mchezo huo umehairishwa hadi hapo utakapopangiwa tarehe nyingine.

Mwambusi alisema kikosi chake ndio kwanza anakisuka anahitaji maandalizi zaidi ili kufikia malengo yake hivyo kuondolewa kwa mchezo huo kumempa nafasi ya kukisuka zaidi.

"Bado natafuta muunganiko wa kikosi nahitaji muda wa kuendelea kukisuka zaidi kwa muda ambao timu yangu ilitakiwa kuchezwa na Yanga naamini nitautumia vyema kuendelea kukinoa kabla ya mchezo wetu na Ruvu Shooting Agosti 22," alisema na kuongeza kuwa.

"Mchezo wa kwanza tumeambulia sare siyo mbaya kwetu tunaendelea kujifua zaidi ili kuhakikisha mchezo ujao tunapata matokeo na tunatarajia kuwa wenyeji hivyo ni vyema zaidi tukaanza kukusanya pointi nyumbani kabla hatujaanza na changamoto ya viwanja vingine," alisema Mwambusi.