Mchongo wa Mwanaspoti wazidi kumwaga zawadi

Muktasari:

Mshindi wa simu, Mwinyihaji aliliambia Mwanaspoti kuwa alikuwa akitumia simu ndogo ambayo hawezi kuperuzi hata katika mitandao ya kijamii na mara baada ya kupata zawadi hiyo maisha yake huko yatabadilika.

WIKI ya sita imeingia tangu promosheni ya Shinda Mchongo na Mwanaspoti ilipoanza Julai Mosi na zawadi zimeendelea kumiminika kwa wasomaji wa Mwanaspoti wanaonunua gazeti na kukata kuponi iliyopo ukurasa wa pili.

Jana Ijumaa ilifanyika droo hiyo ya sita na kupatikana washindi sita akiwamo aliyenyakua simu janja, anayetokea jijini Dar es Salaam.

Aliyenyakua zawadi hiyo ya siku ni Abdul Mwinyihaji, mkazi wa Tuangoma, jijini Dar es Salaam, huku wengine watano wakibeba vitita vya Sh100,000 kila mmoja.

Walioshinda mkwanja huo ni pamoja na Daud Charles wa Mbezi, Msangarufu Mwakasumbula anayetokea Makambako Njombe, Haruna Mohammed anayeishi Temeke na Priscus John wa Magomeni, Dar es Salaam na Fredrick Lamson kutoka Mbeya.

Mshindi wa simu, Mwinyihaji aliliambia Mwanaspoti kuwa alikuwa akitumia simu ndogo ambayo hawezi kuperuzi hata katika mitandao ya kijamii na mara baada ya kupata zawadi hiyo maisha yake huko yatabadilika.

“Nilikuwa naishi kizamani na simu yangu ndogo, lakini Mwanaspoti wamebadilisha maisha yangu kwa kunileta katika utandawazi wa kisasa, hakika sina la kusema nawashukuru kwa ushindi huu ulioniwezesha nami kuwa wa kisasa zaidi,” alisema Mwinyihaji.