Makelele arejea Chelsea

Muktasari:

Gwiji mwingine wa Chelsea, Frank Lampard, amerejea klabuni hapo akiwa kocha mkuu wa timu ya wakubwa.

LONDON, ENGLAND .ENZI inaanza kurudishwa pale Stamford Bridge baada Claude Makelele kutangazwa kuwa atarejea Chelsea akipewa cheo kipya. Kiungo huyo wa zamani anarejea Chelsea kuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa Vijana.
Kazi mpya ya Makelele itakuwa ni kuweka nguvu katika vipaji vinavyoinukia vya klabu hiyo pamoja na wachezaji waliotolewa kwa mkopo.
Pia atakuwa na cheo cha balozi wa Chelsea.
Kwa mujibu wa tovuti ya Chelsea kuna wachezaji 17 waliotolewa kwa mkopo katika klabu mbalimbali.
Kiungo huyo wa kimataifa wa zamani wa Ufaransa, kazi yake itakuwa sawa na ya kipa wao wa zamani, Petr Cech, ambaye yeye atakuwa kwenye timu ya wakubwa. Cech pia ataiongoza klabu hiyo kwenye suala la ufundi.
Gwiji mwingine wa Chelsea, Frank Lampard, amerejea klabuni hapo akiwa kocha mkuu wa timu ya wakubwa.
Hakuna kati ya watatu hao mwenye uzoefu na nafasi aliyopewa kwenye Ligi Kuu, ingawa Lampard alikuwa kocha wa Derby County katika Ligi Daraja la Kwanza msimu uliopita, akiwafikisha kwenye fainali ya mechi za ‘playoff’ ambako walifungwa dhidi ya Aston Villa waliopanda Ligi Kuu wa England.
Makelele aliwahi kufanya kazi katika benchi la ufundi la PSG baada ya kustaafu soka 2011.
Akawa kocha msaidizi PSG 2011-13 chini ya Paul Clement. Kisha akawa kocha mkuu wa Bastia kwa msimu mmoa 2014.