Kazi ni kukafunga tu,sasa kuwa Dr Eliud Kipchoge

Muktasari:

Kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari chuo hicho kilisema kimeamua kumtuza Kipchoge na shahada hiyo kama njia ya kutambua mchango wake mkubwa  kwenye masuala ya sayansi michezo.

Nairobi, Kenya.KUANZIA wiki ijayo, mshikililizi wa rekodi ya dunia kwenye Marathon Eliud Kipchoge atakuwa akiitwa Dr Eliud Kipchoge.

Zikiwa ni siku chache tu baada yake kuibuka na tuzo la Mwanariadha Bora wa Mwaka kwa mara ya pili mfululizo na kisha Rais Uhuru Kenyatta kutoa Sh100 milioni kwa ajili ya ujenzi wa maktaba katika kijiji chake, sasa Chuo Kikuu cha Laikipia kimetangaza kitamvisha shahada ya heshima ya Uzamili.

Ijumaa wiki ijayo chuo hicho kitaandaa makala ya saba ya kufuzu kwa mahafali wake na ni kwenye hafla hiyo ambayo seneti ya Chuo ilipitia  staa Eliud Kipchoge avishwe Shahada ya Utambuzi ya Uzamili katika masuala ya sanyansi (Honorary Degree of Doctor Of Science).

Kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari chuo hicho kilisema kimeamua kumtuza Kipchoge na shahada hiyo kama njia ya kutambua mchango wake mkubwa  kwenye masuala ya sayansi michezo.

“Kwa mujibu wa sehemu ya III (21) (4) (k)  ya chata ya Chuo Kikuu cha Laikipoia inayohusu utoaji wa shahada za utambuzi, seneti inaona heshima kubwa kumtambua Bwana Eliud Kipchoge na Shahada ya Utambuzi katika masuala ya Sayansi wakati wa makala yetu ya saba ya kufuzu kwa mahafala,” taarifa hiyo ilieleza.

Mwezi uliopita Rais Uhuru Kenyatta alimtuza na tuzo  la heshima nchini la Elder of the Order of the Golden Heart of Kenya (E.G.H) kwenye sherehe za Mashujaa Dei.

Mazuri yote haya yamekuwa yakimwandama Kipchoge tangu awe binadamu wa kwanza kukimbia Marathon kwa chini ya saa mbili kule Vienna, Austria mwezi uliopita.