Kocha Stars aguswa na kifo cha Mkapa

Muktasari:

Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, John Pombe Magufuli ametangaza siu saba za maombolezo huku  siku tatu kuanzia kesho Jumapili hadiu Jumanne zikituma kwa watanzania wote kumuaga marehemu Mkapa.

Kocha mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania, Ettiene Ndayiragije ametoa pole kwa watanzania wote kwa kuondokewa na Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamini William Mkapa huku akiwataka kuyaenzi yote mema aliyoyaacha.
Ndayiragije raia wa Burundi amesema hakuna kitu kikubwa kama mtu akifa huku akiwa kaacha alama na ndicho kilichotokea kwa Mkapa ambaye ameacha alama ya Uwanja mkubwa wa Taifa.
Alisema Mkapa anatakiwa kuenziwa ikiwemo kujenga viwanja vingine vya michezo ili kuinua vipaji mbalimbali zilivyopo hapa nchini.
"Natoa pole kwa wote wakiwemo wadau wa mpira kwani huu msiba unatuhusu wote.Ni vizuri tumuenzi na kuendeleza kile amefanya ikiwemo kujenga viwanja vingi kama vile yeye alivyofanikisha ujenzi wa uwanja wa Taifa.
"Hakuondoka tu ila amecha jina na kumbukumbu ya uwanja ambayo kama nchi tunajivunia.Hata timu kutoka nje huwa akifika na kuona uwanja wanausifia ulivyo mkubwa na mzuri.Hivyo jina lake litaendelea kukumbukwa milele"amesema Ndayiragije.
Rais Mstaafu Mkapa alifariki usiku wa kuamkia jana Ijumaa na anatarajiwa kuzikwa  Jumatano katika kijiji cha Lupaso Wilayani Masasi mkoani Mtwara