Mtoto wa Messi shabiki kindandaki wa Ronaldo

Muktasari:

Messi, alikiri mwanae mkubwa ni shabiki wa mpinzani wake mkubwa kwenye Ballon d’Or Ronaldo.

BARCELONA, HISPANIA. SUPASTAA wa Barcelona, Lionel Messi amefichua mwanaye mkubwa, Thiago ni shabiki mkubwa wa Cristiano Ronaldo.
Mtoto huyo, Thiago mwenye umri wa miaka saba, amekuwa akimkosoa baba yake hadharani anapocheza vibaya, mara kwa mara amekuwa akimuulizia baba yake kuhusu staa wa Juventus, Ronaldo.
Staa huyo wa Barcelona ana watoto watatu, Thiago, Mateo na Ciro ambao amezaa na mkewe kipenzi mrembo Antonella Roccuzzo.
Messi, alikiri mwanae mkubwa ni shabiki wa mpinzani wake mkubwa kwenye Ballon d’Or.
Messi alisema: “Anawazungumzia sana Luis (Suarez), ambaye tumekuwa na uhusiano mzuri na amekuwa akiwazungumzia pia Antoine Griezmann na Arturo Vidal tangu siku ya kwanza kutokana na nywele zake.
“Kuhusu watu wa nje ya Barca, amekuwa akiwazungumzia Kylian Mbappe, Cristiano Ronaldo, Neymar. Thiago anawafahamu vizuri wote hao na amekuwa akiuliza maswali mengi sana.”
Kuhusu mtoto wake wa pili, Mateo, 4, yupo tofauti, alionekana wazi kumshangilia baba yake baada ya kumshinda Ronaldo kwenye tuzo ya Ballon d’Or 2019.