Spurs yainyatia Chelsea kwa Simons
Muktasari:
- Nyota huyo wa RB Leipzig, Simons, 22, alikuwa anatarajiwa kuhamia Stamford Bridge baada ya jitihada za mazungumzo kufikia hatua nzuri.
LONDON, ENGLAND: KITENDO cha Chelsea kuchelewa kukamilisha usajili wa kiungo wa RB Leipzig, Xavi Simons kunaweza kufungua fursa kwa Tottenham kuingilia dili hilo na kufanya uhamisho wa dakika za mwisho.
Nyota huyo wa RB Leipzig, Simons, 22, alikuwa anatarajiwa kuhamia Stamford Bridge baada ya jitihada za mazungumzo kufikia hatua nzuri.
Hata hivyo, Chelsea inaonakana kuchelewa huku siku zikiwa zimebakia chache kabla ya dirisha la usajili kufunga Jumatatu ya wiki ijayo.
Tovuti ya The Sun, imefichua kwamba Chelsea inahitaji kwanza kuuza wachezaji zaidi ili kupata pesa za kufanyia usajili huo hali inayozua shaka ya dili hilo kufeli.
Tottenham imekuwa ikitafuta namba 10 mpya katika dirisha hili la majira ya kiangazi na ilijaribu kuwasajili Morgan Gibbs-White na Eberechi Eze lakini wote iliwakosa..
Inaelezwa kwamba Spurs inataka kuhamishia nguvu zao kwa Simons ambaye Spurs ipo tayari kumuuza kabla ya mwezi huu kumalizika.
Mchezaji huyo wa kimataifa wa Uholanzi anadaiwa kupendelea kuhamia Chelsea, lakini iwapo uhamisho huo hautatimia, huenda akalazimika kuzingatia dili hilo la Spurs.
Inadaiwa anahitaji mshahara mkubwa ili kutua timu yoyote ile inayomhitaji wakati Leipzig ikihitaji Pauni 60 milioni kama ada yake ya uhamisho.
Mbali ya Simons, Spurs pia inataka kufanya jitihada za kuhakikisha inampata mchezaji wa Monaco, Maghnes Akliouche, 23, ambaye juzi (Jumatano) aliitwa kwa mara ya kwanza katika kikosi cha taifa la Ufaransa.