De Gea anukia Saudia
Muktasari:
- De Gea ambaye aliondoka Man United katika dirisha lililopita la majira ya kiangazi baada ya kudumu kwa zaidi ya miaka 10, amekuwa nje ya uwanja tangu kuanza kwa msimu huu baada ya kukosa timu.
RIYADH, SAUDI ARABIA: KIPA wa zamani wa Manchester United, David de Gea ameripotiwa kuwa kwenye mazungumzo na Al Shabab ya Saudi Arabia kwa ajili ya kujiunga nayo katika dirisha hili.
De Gea ambaye aliondoka Man United katika dirisha lililopita la majira ya kiangazi baada ya kudumu kwa zaidi ya miaka 10, amekuwa nje ya uwanja tangu kuanza kwa msimu huu baada ya kukosa timu.
Awali, mashetani wekundu walikuwa na mpango wa kutaka kumsainisha mkataba mpya ambao ungempunguzia mshahara wake wa Pauni 375,000 kwa wiki na De Gea akakubali lakini baadaye wakasitisha na kumsajili Andre Onana kutoka Inter Milan ili achukuwe nafasi yake.
Tangu hapo kipa huyu amekuwa akihusishwa na timu nyingi za Saudia na barani Ulaya ikiwa pamoja na Al-Nassr.
Ikiwa itafanikisha mchakato wa kumpata De Gea inaweza kuwasaidia Al Shabab kuboresha zaidi kikosi chao kwani hadi sasa inaye Ivan Rakitic iliyemchukua kutoka Sevilla pia inapambana kuipata huduma ya staa wa Newcastle, Miguel Almiron na winga wa Chelsea, Hakim Ziyech ambaye anacheza kwa mkopo Galatasaray.
Al-Shabab kwa sasa inashika nafasi ya 11 kwenye msimamo wa Ligi Kuu nchini Saudi Arabia na imeshinda mechi moja tu kati ya saba za mwisho.
Hata hivyo, inadaiwa kuwa haitakuwa rahisi kwa wababe hawa kumsajili De Gea kwa sababu kipa huyu bado ana mpango wa kutaka kuendelea kucheza soka la kiushindani barani Ulaya, ingawa pesa nyingi inaweza kumbadili.