Yanga yapunguzwa kasi, mashabiki wawa mbogo

Muktasari:

Yanga imetoka suluhu na Namungo katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliofanyika Leo kwenye  uwanja wa Majaliwa Ruangwa Lindi huku mashabiki wa timu hiyo wakigeuka mbogo  baada ya mwamuzi kukataa bao lililofungwa na Yacouba Sogne.

Yanga imetoka suluhu na Namungo katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliofanyika Leo kwenye  uwanja wa Majaliwa Ruangwa Lindi huku mashabiki wa timu hiyo wakigeuka mbogo  baada ya mwamuzi kukataa bao lililofungwa na Yacouba Sogne.


Sogne amefunga bao hilo kwa kichwa akimalizia Kona ya Said Ntibazonkiza 'Saido' lakini wakati mwamuzi wa Kati Hance Mabena akiashiria kukubali mshika kibendera namna moja, Abdulaziz Ali wa Arusha alinyoosha kibendera huku ikishindwa kufahamika kama aliashiria mfungaji  ameotea au Mpira ulitoka.
Baada ya filimbi ya mwisho ya mwamuzi mashabiki wa Yanga walianza kufoka kwa hasira wakidai mwamuzi amewaonea kwani bao lilikuwa halali kabisa.


"Yaani hawa  waamuzi wanazingua sana,sasa lile bao refa amelikataa kuna kosa gani, yaani hawa waamuzi wanatia hasira sana, wachezaji wanapambana wanafunga wao wanakuwa na matokeo yao,"amesema shabiki maarufu anayefahamika kama Mark Yanga huku akifoka kwa hasira.
Yanga itabidi wajilaumu wenyewe kushindwa kushinda mchezo huo  kwani licha ya kufika mara nyingi golini kwa Namungo lakini  washambuliaji wao walishindwa kutumia vizuri nafasi walizopata.


Timu zote zilianza mchezo  kwa kasi na dakika ya Tano tu Yanga ilifika golini kwa Namungo lakini pasi Safi ya Said Ntibazonkiza 'Saido' ilishindwa kumaliziwa na Michael Sarpong.
Namungo ilijibu mashambulizi dakika ya 8 lakini Hashim Manyanya alishindwa kufunga akiwa katika nafasi nzuri na baada ya kupiga pasi iliyotoka nje kidogo ya lango.


Yanga ilionekana kufanya mashambulizi mengi langoni mwa Namungo  kipindi Cha kwanza lakini washambuliaji wake walioongozwa na Yacouba Sogne na Michael Sarpong walishindwa kuwa na akili ya kumalizia vizuri
Timu hiyo ilikuwa ikitengeneza mashambulizi kupitia kwa Saido na Tuisila Kisinda lakini Kila walipofika golini washambuliaji wa Yanga walishindwa kufanya uamuzi nzuri wa kutumbukiza Mpira wavuni.


Dakika ya 17 Said alipiha Kona ambayo iliokolewa na mabeki wa Namungo huku mrundi huyo akishindwa kufunga dakika ya 22 akiwa katika nafasi nzuri  baada ya kupata pasi ya Tuisila.