Rayvanny kunogesha Tulia Traditional Dance

Muktasari:

Tamasha hilo linafanyika kwa mwaka wa nne, ambapo vikundi vya ngoma mbalimbali kutoka maeneo tofauti hapa nchini hushiriki tukio hilo.

Mbeya. Msanii wa kizazi kipya kutoka rebo ya WCB, Raymond Mwakyusa ‘Rayvanny’ anatarajia kunogesha tamasha la ngoma za asili ‘Tulia Traditonal dance’ linalotarajia kufanyika jijini Mbeya kwa siku tatu mfululizo.

Tamasha hilo linafanyika kwa mwaka wa nne, ambapo lengo lake ni kutangaza vivutio vya utalii kwenye Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, lakini kufungua fursa za kiuchumi.

Akizungumza leo Jumanne Septemba 21, mratibu na mwandaaji wa tamasha hilo, Naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Dk Tulia Akson, amesema tamasha hilo linatarajia kufanyika Alhamisi hadi Jumamosi.

Amesema viongozi mbalimbali wa serikali watakuwapo, ikiwa ni Waziri wa Mali Asili na Utalii, Dk Damas Ndumbaro na Waziri wa Michezo, Sanaa na Utamaduni, Innocent Bashungwa.

“Baada ya mwaka jana kushindwa kufanyika tamasha hili kwa ishu ya ugonjwa wa Uviko 19, mwaka huu limerudi upya na itafanyika kuanzia Septemba 23 hadi 25 kwenye uwanja wa zamani wa ndege jijini hapa” amesema Tulia.

Amesema vikundi mmbalimbali vya ngoma kutoka maeneo mbalimbali hapa nchini vitashiriki na zawadi zitakuwapo kwa washindi ikiwamo pesa taslimu.