Eymael: Nilipiga goti kupinga ubaguzi, sijaambiwa lolote Yanga
Photo credit: Azam TV
Muktasari:
Eymael amefutwa ukocha na Yanga baada ya sauti yake kusambaa akitoa matamshi ya kibaguzi
BAADA ya mabosi wa Yanga kumtimua kocha wao Luc Eymael, kocha huyo amesema suala la yeye kuondolewa kazini bado halijafika rasmi kwake kutokana na hakuna kiongozi yoyote ambaye amewasiliana nae.
Akizungumza na Mwanaspoti Online, Eymael amesema ameona taarifa kwa kiswahili ikisambaa na kutumiwa na watu mbalimbali lakini bado hajapaewa taarifa rasmi.
"Tupo njiani ndio tunarudi huko Dar, mtandao sio mzuri sana lakini nimeona nikitumiwa barua na watu mbalimbali lakini imeandikwa kwa kiswahili kwahiyo sijaelewa lolote mpaka sasa," alisema.
Akizungumzia kuhusu sauti yake akitoa maneno ya kibaguzi kwa mashabiki na wapenda soka nchini, Luc alisema tatizo lilianzia Jumatano Julai 22, 2020 alipokatazwa kufanya mahojiano na waandishi wa habari baada ya mechi yao na Mtibwa Sugar.
"Baada ya ule mchezo kulikuwa na mvutano sana, nilizuiwa kufanya mazungumzo na waandishi wa habari pale uwanjani, na niliporudi hotelini nilisumbuliwa sana, kulikuwa na mwandishi alikuwa ananihoji sana maswali mengi nikamwambia kwamba sipo katika hali nzuri lakini bado alikuwa anaendelea hivo hivo tu,".
"Kama tulikuwa tunajibizana hivi na nilijua kabisa kwamba kabla ya mchezo au baada ya mchezo na Lipuli ingeweza kutokea hili kwa sababu nilikuwa najua nini kinakuja na ndio maana Ijumaa niliomba samahani lakini hawakujua kwanini niliomba".
Aliongeza kwa kusema "Kama ningekuwa mimi ni mbaguzi wa rangi basi nisingeweza kufanya kazi miaka mingi Afrika, pia nisingeweka ishara ya kupinga ubaguzi na ndio maana jana nilipiga goti moja pale uwanjani,”