Aucho, Chama wampa darasa kiungo Coastal
Muktasari:
- Kiungo huyo aliyetua Coastal Union dirisha dogo la Januari 2025, amesema miongoni mwa wachezaji ambao amekuwa akiwaangalia kwa karibu ni Aucho ambaye anaamini amejenga jina kubwa kutokana na uthabiti wa kiwango na uwezo wa kutawala eneo la katikati ya uwanja.
KIUNGO mkabaji wa Coastal Union, Luician Kilua amewataja viungo Khalid Aucho wa Singida Black Stars na Clatous Chama wa Simba kuwa ni nyota anaowaangalia huku akipata darasa kwa namna wanavyocheza na kuendesha mchezo ndani ya uwanja.
Kiungo huyo aliyetua Coastal Union dirisha dogo la Januari 2025, amesema miongoni mwa wachezaji ambao amekuwa akiwaangalia kwa karibu ni Aucho ambaye anaamini amejenga jina kubwa kutokana na uthabiti wa kiwango na uwezo wa kutawala eneo la katikati ya uwanja.
Kiungo huyo amesema, Aucho si aina ya viungo wanaotegemea nguvu pekee, bali ana uwezo mkubwa wa kusoma mchezo, kupanga kasi ya timu na kubaki mtulivu hata kwenye mechi zenye presha kubwa.
“Kwa Ligi ya Tanzania nampenda sana Khalid Aucho. Ni mmoja wa viungo bora ambao wamewahi kucheza kwenye Ligi Kuu Bara. Kuna mambo mengi nimekuwa nikijifunza kwake hasa namna anavyosimamia eneo la kiungo kwa utulivu na nidhamu,” amesema kiungo huyo.
Mbali na Aucho aliyewahi kuichezea Yanga, Kilua alimtaja Chama kuwa mmoja wa mastaa ambao wameendelea kumvutia kutokana na uwezo wa kubeba majukumu makubwa ndani ya timu na kuendelea kuwa na kiwango kizuri kwa muda mrefu.
Amesema Chama mwenye mabao manane yakiwemo sita aliyofunga ndani ya Simba ambayo aliyoanza kuitumikia dirisha dogo msimu huu, ameweza kujenga heshima ndani ya soka la Tanzania si kwa bahati, bali kupitia kazi, kujitunza na nidhamu ambayo imemfanya aendelee kuwa na ushawishi kila msimu.
“Kwa mtazamo wangu si rahisi kwa mchezaji kuendelea kuwa na ushawishi kila msimu bila kuwa na nidhamu na kujitunza. Namkubali sana Chama, ana uwezo mkubwa wa kuisaidia timu kupata matokeo na ni miongoni mwa mastaa wanaolinda kiwango chao kwa kufanya kazi kila siku,” amesema.