Mwaikimba aibukia New Fighter ya Kyela

Kyela.Baada ya kupotea kwa muda uwanjani, hatimaye Straika wa zamani wa Yanga, Azam na timu ya Taifa 'Taifa Stars',  Gaudence Mwaikimba leo ameibukia New Fighter FC inayoshiriki Ligi ya Wilaya ya Kyela.

Nyota huyo mbali na kung'ara na timu hizo kubwa nchini, pia alizitumikia Boma FC, Arusha United na Pamba FC kwa mafanikio.

Leo katika mashindano maalumu yanayozishirikisha timu za Mkoa wa Mbeya, nyota huyo ameonekana akiwa na kitambaa cha Unahodha akiitumikia New Fighter ambayo inajiandaa na daraja la nne Wilaya ya Kyela.

Timu hiyo ilikuwa ikimenyana na Mbeya City ambazo zipo kundi moja A, ambapo kila upande unapambana kusaka ushindi ili kujiweka maizngira mazuri ya kufuzu nusu fainali.

Katika kundi hilo, timu hizo zimechezea vichapo, ambapo New Fighter walilala mbele ya Small Boys bao 1-0, huku Mbeya City wakikwama kwa ndugu zao, Mbeya Kwanza na kujikuta wakijiweka pabaya.

Hata hivyo hadi sasa wakati mchezo huo ukiwa mapumziko, Mbeya City wanaongoza bao 1-0 lililofungwa na Helbert Lukindo dakika ya 11 na kufufua matumaini ya kuweza kufuzu hatua inayofuata.