Chama aiteka Sokoine, kuikosa Mbeya City

Chama aiteka Sokoine, kuikosa Mbeya City

Muktasari:

  • Chama licha ya kutajwa zaidi uwanjani hapo, lakini aliishia kuwapungia mkono mashabiki  na kubaki kwenye gari bila kuungana na wenzake walioingia vyumbani kubadilisha nguo tayari kwa mechi dhidi ya Mbeya City.

Mbeya. ''Chama, Chama, Chama, Chama''. Ni shangwe na kelele zilizosikika kwa mashabiki wakimlaki nyota wao raia wa Zambia, Clatous Chama wakati Simba ikiwasili uwanja wa Sokoine tayari kwa mchezo wao dhidi ya Mbeya City.

Shangwe hizo zilitokea wakati timu hiyo ikitua kwa ajili ya maandalizi ya mwisho kuwakabili wenyeji Mbeya City katika mchezo wa Ligi Kuu utakaopigwa saa 10:00 jioni.

Mbeya City ndio walitangulia kutua saa 7:44 mchana bila amsha amsha yoyote wakipigiwa makofi na mashabiki wao hadi vyumba vya kubadilishia nguo.

Saa 8:17 Simba ilitinga uwanjani hapo ikiongozwa na gari la Polisi na kuamsha mzuka uliojaa shangwe kwa mashabiki walianza kuliimba jina la Mwamba huyo wa Lusaka.

Hata hivyo katika sura zilizoshuka kwenye gari la wachezaji, staa huyo hakuwa miongoni lakini viongoni walinong'onezana na kumshusha nje ili kuwapungia mkono mashabiki.

Hatua hiyo iliamsha yowe kwa wakereketwa hao waliojaa jukwaani wakishangilia, huku Afisa Habari wa timu hiyo, Ahmed Ally naye akiongeza mzuka kwa mashabiki.