Prime
Rekodi zinavyoipa Yanga kibarua kizito CAF
UHONDO wa hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika, utaanza rasmi Novemba 21, 2025, ambapo wawakilishi wa Tanzania, Yanga na Simba wameshajua wapinzani wao, baada ya droo kufanyika Novemba 3, 2025 jijini Johannesburg, Afrika Kusini.
Yanga imepangwa kundi B, ikiwa na Al Ahly kutoka Misri, AS FAR (Morocco) na JS Kabylie ya Algeria, huku kwa upande wa Simba ikiangukia kundi D, sambamba na klabu za Esperance de Tunis ya Tunisia, Petro de Luanda (Angola) na Stade Malien ya Mali.
Yanga inayonolewa na Mreno, Pedro Goncalves, ilianza Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuitoa Wiliete De Benguela ya Angola kwa jumla ya mabao 5-0, kisha kuitupa nje Silver Strikers kutoka Malawi kwa jumla ya mabao 2-1 na kufuzu makundi.
Wakati miamba hiyo inayowakilisha Tanzania katika Ligi ya Mabingwa Afrika msimu wa 2025-2026 ikitambua wapinzani wao, Mwanaspoti linakuletea wasifu wa kundi B la Yanga, ambalo lina timu tatu za ukanda wa Kaskazini mwa Bara la Afrika.
AL AHLY (MISRI)
Timu hii iliyoanzishwa Aprili 24, 1907, ikiwa na miaka 118, sasa ndio mabingwa wa kihistoria wa michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika. Kikosi hicho kinachonolewa na kocha Jess Thorup, kimechukua taji hilo mara 12 hadi sasa.
Al Ahly imechukua taji hilo mwaka 1982, 1987, 2001, 2005, 2006, 2008, 2012, 2013, 2019-20, 2020-21, 2022-23 na 2023-24, huku katika Kombe la Shirikisho Afrika ikilichukua taji mara moja, baada ya kufanya hivyo mwaka 2014.
Katika Ligi Kuu ya Misri, Al Ahly imechukua ubingwa mara 45, pia ikibeba Kombe la Misri mara 39, Egyptian Super Cup mara 15, Sultan Hussein Cup (7), Cairo League (16), United Arab Republic Cup (1) na African Cup Winners’ Cup mara nne.
Makombe mengine ni CAF Super Cup (8), Afro-Asian Cup (1), Arab Club Champions Cup (1), Arab Cup Winners’ Cup (1), Arab Super Cup (2), FIFA African-Asian-Pacific Cup (1) na Egyptian Club Champions Cup (1). Ina jumla ya mataji 155.
Al Ahly sio wageni wa Yanga katika michuano hii, kwa sababu zimeshakutana ambapo hivi karibuni ilikuwa ni msimu wa 2023-24, kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika zikiangukia kundi D na kumaliza ya kwanza na ya pili, hivyo zikafuzu robo fainali.
Msimu huo, mechi ya kwanza jijini Dar es Salaam, Yanga ililazimishwa sare ya kufungana bao 1-1, Desemba 2, 2023, huku ya marudiano iliyopigwa Cairo nchini Misri, wenyeji Al Ahly walishinda kwa 1-0, lililofungwa na Hussein El Shahat, Machi 1, 2024.
Katika msimu huo, Al Ahly ilimaliza kinara na pointi 12, ikiungana na Yanga iliyomaliza ya pili kwa pointi nane sawa na CR Belouizdad ya Algeria iliyomaliza ya tatu kwa tofauti ya mabao, huku Medeama ya Ghana ikiburuza mkiani kwa pointi nne.
Yanga ilifika hadi robo fainali na kutolewa na Mamelodi Sundowns ya Afrika Kusini kwa penalti 3-2, baada ya suluhu (0-0) mechi zote mbili, huku Al Ahly ikichukua taji hilo kwa kuichapa Esperance de Tunis ya Tunisia kwa jumla ya bao 1-0.
AS FAR (MOROCCO)
Miamba hii ambayo jina kamili ni Association Sportive des Forces Armees Royales au la utani ‘Al-Zaeem’ yaani The Bosses, kwa sasa inanolewa na kocha Alexandre Santos, raia wa Ureno, ambapo kikosi hicho kimeanzishwa Septemba 1, 1958.
AS Far iliyotimiza miaka 67 tangu kuanzishwa kwake, imechukua mataji mbalimbali, ambapo katika Ligi Kuu ya Morocco ‘Botola Pro’ imechukua 13, kuanzia mwaka 1961, 1962, 1963, 1964, 1967, 1968, 1970, 1984, 1987, 1989, 2005, 2008 na 2023.
Moroccan Throne Cup imechukua mara 12 (1959, 1971, 1984, 1985, 1986, 1999, 2003, 2004, 2007, 2008, 2009 na 2020), huku Moroccan Super Cup, ikichukua manne (1959, 1961, 1962 na 1963) na Ligi ya Mabingwa Afrika ilichukua mara moja 1985.
Mataji mengine ni Kombe la Shirikisho Afrika mwaka 2005 na Botola 2 ikichukua mara moja pia mwaka 1959, ambapo timu hiyo inashiriki Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara ya 14, huku mafanikio iliyoyapata ni kuchukua ubingwa huo mwaka 1985.
Mafanikio mengine ni kufika nusu fainali ya Kombe la Ligi ya Mabingwa Afrika mwaka 1968 na 1988, huku ikiwa ni timu ya kwanza kutoka Morocco kushiriki Kombe la Afrika na ya kwanza pia kwa nchi hiyo kuchukua ubingwa wa mashindano hayo mwaka 1985.
Katika Kombe la Shirikisho Afrika, imeshiriki mara saba, huku mafanikio makubwa ni kuchukua ubingwa huo mwaka 2005 na kufika fainali 2006, ilipokosa taji mbele ya Etoile du Sahel ya Tunisia kwa faida ya bao la ugenini baada ya sare ya 1-1.
Kwenye Kombe la Washindi Afrika, timu hiyo imeshiriki mara tano, mafanikio makubwa ni kufika fainali mwaka 1997, ikifika robo fainali mara tatu 1987, 1999 na 2000, huku mwaka uliofuatia wa 2001, ikitolewa mapema tu raundi ya pili.
Pia, ilifika hadi fainali ya CAF Super Cup 2006 na kukosa taji hilo, ambapo kikosi hicho kilishindwa kutamba mbele ya Al Ahly ya Misri, baada ya kuchapwa kwa penalti 4-2 kufuatia kutoka suluhu (0-0), mechi iliyopigwa Februari 24, 2006.
JS KABYLIE (ALGERIA)
Jeunesse Sportive de Kabylie au jina la utani la ‘The Canaries’, ni timu ya Algeria iliyoanzishwa Agosti 2, 1946, ikitimiza miaka 79, ambapo kwa sasa kikosi hicho chenye historia kubwa kiko chini ya Kocha, Mjerumani Josef Zinnbauer.
Timu hiyo hadi sasa ina mataji 14 ya Ligi Kuu ya Algeria, kuanzia 1972-73, 1973-74, 1976-77, 1979-80, 1981-82, 1982-83, 1984-85, 1985-86, 1988-89, 1989-90, 1994-95, 2003-04, 2005-06 na mara ya mwisho ni 2007-08.
Algerian Cup imechukua mara tano, 1976-77, 1985-86, 1991-92, 1993-94 na 2010-11, huku Algerian League Cup ikichukua mara moja msimu wa 2020-21, sawa na ilivyokuwa pia Algerian Super Cup ililochukua mwaka 1992.
Taji la Ligi ya Mabingwa Afrika imliechukua mara mbili, 1981 na 1990, African Cup Winners’ Cup imechukua 1995, CAF Cup mara tatu kuanzia 2000, 2001 na 2002 ikiwa ni rekodi kwa timu hiyo inayoshiriki Ligi ya Algeria maarufu ‘Algerian Ligue Professionnelle 1’.