UDSM, DAR City zachuana BDL

Muktasari:

  • Timu hizo zilianza kuchuana tangu ligi ilivyoanza Machi 3 mwaka huu. 

Timu ya Dar City na UDSM Outsiders, zinakabana koo katika uongozi wa Ligi ya Kikapu ya Mkoa wa Dar es Salaam (BDL)inayoendelea kwenye Uwanja wa Donbosco, Oysterbay, Dar es Salaam.

Timu hizo zilianza kuchuana tangu ligi ilivyoanza Machi 3 mwaka huu. 

Mabingwa watetezi wa ligi hiyo, Dar City,  ndiyo wanaongoza katika kwa pointi 25 kutokana na michezo 13 waliyocheza,  wakipoteza mchezo mmoja.

Inayofuatia ni timu ya UDSM Outsiders yenye pointi 24 baada ya kucheza michezo 12, huku timu hiyo hadi sasa ikiwa haijapoteza mchezo wowote. 

Wakati timu hizo zikichuana vikali pale kileleni mwa msimamo, Savio, Mchenga Stars, Vijana ‘City Bulls’, ABC na JKT zinazifuatia kwa karibu.

Michezo iliyochezwa Jumapili usiku, timu ya UDSM Outsiders iliishinda Mgulani (JKT) kwa pointi 43-40, Dar City ikishinda 97-53 dhidi ya Ukonga Kings na Savio ikiibwaga Vijana 75-69.