Pacome afunga bandeji goti aliloumia

Muktasari:

  • Pacome aliumia Machi 17 katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Azam FC ambao Yanga ilipoteza kwa mabao 2-1.

LICHA ya kuonekana kuwa fiti kwa ajili ya mchezo wa robo fainali ya kombe la shirikisho (FA), kiungo wa Yanga, Pacome Zouzoua ameonakana akiwa amefunga bandeji ya bluu kwenye goti aliloumia zaidi ya mwezi mmoja uliopita.

Pacome aliumia Machi 17 katika mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Azam FC ambao Yanga ilipoteza kwa mabao 2-1.

Fundi huyo mwenye mabao saba katika ligi, ameonekana  wakati wa mazoezi mepesi kwa ajili ya mchezo wa robo fainali ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Tabora United kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi, usiku huu.

Muivory Coast huyo alikuwa akipasha na  kundi la wachezaji wa akiba akiwemo Farid Mussa, Kennedy Musonda na Joseph Guede ambao waliunda duara huku aliyekuwa katikati akiwa na jukumu la kukaba ili kupokonya  mpira.

Zouzoua alionekana kuwa mwepesi huku akifanya kwa nguvu zoezi hilo na mara kadhaa alionekana kujinyoosha na wakati mwingine aliruka juu ikiwa ni sehemu ya kufanya zaidi ya kile ambacho wenzake walikuwa akifanya.

Kikosi cha Yanga kilichoanza; Djigui Diarra, Kibwana Shomary, Nickson Kibabage, Ibrahim Hamad 'Bacca', Bakari Mwamnyeto, Khalid Aucho, Mudathir Yahya, Shekhan Ibrahim, Clement Mzize, Stephane Aziz KI na Max  Nzengeli.