Mabao yaliyozua furaha na uchungu TPL

RAHA ya mechi bao wala usibishe. Mpaka sasa mambo yanazidi kunoga Ligi Kuu Tanzania Bara huku mabao ya maana yakifungwa na Yanga ikiwa kinara katika msimamo wa Ligi Kuu ikiwa na pointi 67 baada ya kucheza meichi 28 kabla mechi ya jana Alhamisi.

Kama kawaida ya Mwanaspoti linakuletea baadhi ya mabao ambayo yamepachikwa katika dakika za lala salama na kuzua furaha huku wengine wakibaki na majonzi.

ALEX KITENGE v YANGA

Ni mmoja kati ya mchezo ambao utakumbukwa kwa mengi na mashabiki wa soka kutokana na ushindani jinsi ulivyokuwa siku hiyo pale Uwanja wa Taifa kati ya Yanga na Stand United.

Mchezo huu ulipigwa Septemba 16 na Yanga iliyokuwa mwenyeji iliibuka na ushindi wa mabao 4-3 yaliyofungwa na Mrisho Ngassa, Ibrahim Ajibu, Deus Kaseke pamoja na Andrew Vincent ‘Dante’. Ni mchezo wa kwanza kuzalisha hat trick Ligi Kuu ambayo iliwekwa na Alex Kitenge dakika ya 15, 59 na bao la mwisho akipiga dakika za nyongeza na kuipa presha Yanga huku langoni kipa akiwa, Klaus Kindoki.

KINDAKI v PRISONS

Ulikuwa mwezi wa majanga kwa timu kuachia pointi dakika za mwishoni. Mshambuliaji wa Mbao FC, Robert Kindaki aliihakikishia timu yake inabakisha alama tatu nyumbani katika mchezo uliopigwa Septemba 24. Zikiwa zimesalia sekunde chache huku Prisons ikiamini itaondoka na alama moja ugenini lakini mambo yakabadilika kwa bao la Kindaki.

IBRAHIM AJIBu v MBAO

Dakika ya 16, Raphael Daudi aliiweka kifua mbele Yanga dhidi ya Mbao FC. Naye Ibrahim Ajibu akifunga bao la pili katika dakika za majeruhi. Wakati Ajibu akifanya yake siku hiyo (Oktoba 7). Juhudi Philemon naye aliinasua Alliance kutoka kwenye kichapo baada ya kusawazisha dakika za nyongeza na mchezo kumalizika kwa sare ya bao 1-1 baada ya Abdulrahman Mussa kuiweka mbele JKT Tanzania dakika ya 70. Lameck Chamkanga wa Biashara naye alirahisisha kazi kwa Mwadui alipojifunga dakika ya 89 katika harakati za kuokoa na kuifanya Mwadui kuibuka na ushindi wa mabao 2-0.

ZABRON HAMIS v SIMBA

Mchezo wa pili kuzaa hat trick pale Emmanule Okwi aliponogesha ushindi wa maboa 5-1 dhidi ya Alliance baada ya mabao mengine ya Asante Kwasi na Adam Salamba. Hata hivyo, Simba ikiamini itamaliza dakika 90 bila nyavu zao kuguswa, Zabrona Khamis aliichambua ngome ya Simba na kuachia mkwaju mkali uliomshinda Aishi Manula.

MUJWAHUKU v MBEYA CITY

Jamaa alipindua meza kibishi unaambiwa. Hadi dakika ya 80 Mbao FC iliyokuwa nyumbani ilikuwa imepigwa 2-0 mabao ya Iddy Selemani (11), na Eliud Ambokile (48). Evaligestus Mujwahuki akaikomboa Mbao FC kwa mabao yake ya dakika 83 na lile la dakika za nyongeza na ngoma kumalizika kwa sare ya mabao 2-2 jambo lililowafurahisha Mbao na kuwa machungu kwa Mbeya City.

KIGGI v SINGIDA UNITED

Ilikuwa siku njema kwa mkali huyo wa Alliance alipoihakikishia timu yake kubaki na alama tatu nyumbani baada ya kungoja hadi dakika za nyongeza iliopoibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Singida United.

Naye Jaffar Kibaya alinogesha ushindi wa mabao 4-0 wakati Mtibwa ikiiadhibu Ruvu huku Kibaye baada ya kurudi kambani dakika za nyongeza siku hiyo.

AMISS TAMBWE v PRISONS

Tanzania Prisons ikiwa Uwanja wa Sokoine ilikwenda mapumziko ikiwa kifua mbele kwa bao la Jumanne Elfadhil kupitia mkwaju wa penalti. Yanga ilirejea dakika 45 za kipindi cha pili kusaka ushindi katika mchezo huo ulioshuhudia kadi nyekundu za Mrisho Ngassa (Yanga) na Laurian Mpalile (Prisons). Ajibu alijibu mapigo dakika ya 76 kabla ya Tambwe aliyetokea benchi kutupia dakika ya 85 na dakika za nyongeza na kuondoka na ushindi wa mabao 3-1.

WENGENE HAWA HAPA

Said Dilunga naye alitupia moja Ruvu ilipolala dhidi ya Lipuli 2-1, Steven Mganga alitupia mbili kwenye ushindi wa 2-0 Lipuli FC dhidi ya Mbeya City.

Makambo aliipaisha Yanga ilipoilaza 3-2 Ruvu, David Mwasa aliiokoa KMC kwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Mbao FC na Hafidh Mussa akaibeba Stand United kwenye sare ya bao 1-1dhidi ya Alliance FC.