Essien amtia neno Hazard kuhusu Madrid

Muktasari:

  • Eden Hazard ameambiwa abaki tu Chelsea na kutimiza ndoto zake akiwa hapo ili aachane na habari za kwenda Real Madrid

LONDON, ENGLAND, SUPASTAA, Eden Hazard ameaswa kwamba asishawishike na mpango wa kwenda kujiunga na Real Madrid na badala yake abaki Chelsea mahali ambako thamani na heshima yake imekuwa kubwa zaidi.
Kiungo wa zamani wa wababe hao wa Stamford Bridge, Michael Essien amemwambia Hazard kwamba anaamini atalifikiria kwa kina zaidi suala la kwenda kujiunga na Real Madrid wakati watakapokuja kuifukuzia saini yake kwenye dirisha la usajili la Januari na lile la mwisho wa msimu.
Hazard mwenyewe amekiri kwamba ndoto zake ni kwenda kuichezea Real Madrid na jambo hilo ndilo linalomfanya achelewe kukubali kusaini mkataba mpya kwenye kikosi cha Chelsea ambao utamshuhudia akilipwa Pauni 300,000 kwa wiki.
Essien, ambaye alishinda mataji tisa katika misimu minane aliyodumu na Chelsea, aliwahi kuichezea Real Madrid kwa mkopo katika msimu wa 2012-13 wakati timu hiyo ilipokuwa chini ya kocha Jose Mourinho.
Alisema: “Eden yupo na furaha Chelsea. Na hilo unaweza kuliona kwa msimu mzuri aliokuwa nao. Tunaamini ataendelea hivyo hadi mwisho wa msimu na atabaki hapo kwa muda mrefu zaidi."
Essien amekuwa mchezaji huru tangu Machi na amekuwa akifanya mazoezi na kikosi cha akiba cha Chelsea akisubiri timu ije kumsajili.