De Ligt afanya uamuzi, anakwenda Juventus

TURIN, ITALIA. BEKI wa kati wa Ajax, Mdachi Matthijs de Ligt ameshadanya uamuzi wa timu gani ya kujiunga nayo kwenye dirisha hili la uhamisho wa majira ya kiangazi huko Ulaya baada ya kusakwa na Manchester United, Juventus na Barcelona.


Beki huyo ameripotiwa kuzipiga chini Man United na Barcelona na kuamua kujiunga na Juventus kwa mujibu wa taarifa za kutoka Uholanzi.


Man United ilikuwa ikimsaka sana beki huyo huku kukiwapo na taarifa kwamba angeenda Barcelona wakati huo huo kukiwa na ripoti nyingine zilizokuwa zikimhusisha na mpango wa kwenda kujiunga na Paris Saint-Germain.


Lakini, sasa kinachoelezwa ni kwamba Juventus wameonekana kushinda vita hiyo ambapo wamedaiwa watambeba De Ligt kwa dau la Pauni 62 milioni na kumaliza utata wote wa beki hiyo atakwenda wapi kwenye dirisha hili la majira ya kiangazi.


Hivi karibuni, kwenye fainali ya Uefa Nations League baina ya Ureno na Uholanzi kuripotiwa kwamba supastaa Cristiano Ronaldo, anayekipiga kwenye kikosi cha Juventus alimshauri beki huyo kinda kwenda kujiunga na wababe hao wa Italia, ambao kuanzia msimu unao watakuwa chini ya kocha Maurizio Sarri.


De Ligt alikuwa kwenye kiwango bora kabisa msimu uliopita wakati alipoisaidia Ajax kufikia nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya huku wakibeba mataji ya ligi  za ndani huko Uholanzi, ikiwamo taji la Ligi Kuu Uholanzi.