Crouch aitabiria makubwa Spurs

Muktasari:

Crouch alisema licha ya Spurs kuwaduwaza wengi wa kutosajili mchezaji hata mmoja katika dirisha la usajili wa kiangazi, lakini kwa ubora wa kikosi ilichonacho anaamini itamaliza ndani ya nne bora.

London, England. Mshambuliaji wa Stoke City, Peter Crouch ameitabiria mema timu ya Tottenham Hotspur katika msimu huu wa Ligi Kuu England.

Crouch alisema licha ya Spurs kuwaduwaza wengi wa kutosajili mchezaji hata mmoja katika dirisha la usajili wa kiangazi, lakini kwa ubora wa kikosi ilichonacho anaamini itamaliza ndani ya nne bora.

Alisema klabu hiyo ya Kaskazini mwa London, itaendelea kuwa na ubora ule ule iliokuwa nao msimu uliopita kwa sababu kikosi chake cha kwanza hakijabadilika.

“Binafsi naitabiria Spurs mafanikio msimu huu, licha ya kuwa haijasajili mchezaji yeyote lakini imefanya vizuri kwa kutouza mchezaji yeyote wa kikosi chake cha kwanza,” alisema Crouch.

Mshambuliaji huyo alisema mbali ya Spurs timu nyingine anazozitabiria kumaliza ndani ya nne bora ni Liverpool, Manchester City na Manchester United, wakati Chelsea na Arsenal akizipa nafasi zile zile za msimu uliopita.