Wanauzwa 10, aje Griezmann Barca

BARCELONA, HISPANIA

BARCELONA inapiga mnada wa mastaa wake kibao kwenye dirisha lijalo la usajili ili tu kupata pesa kwa ajili ya kukamilisha dili na masupastaa inaowataka watue kwenye kikosi chake.

Kiungo wa Ajax, Frenkie de Jong tayari ameshatua kwenye timu hiyo kwa ada ya Pauni 67 milioni na wababe hao kwa sasa wanaapiga hesabu za kumchukua beki Matthijs de Ligt kwa Pauni 65 milioni kutoka kwenye kikosi hichohicho cha mabingwa wa Uholanzi.

Antoine Griezmann alitangaza hivi karibuni kuondoka Atletico Madrid na kinachoelezwa ni kwamba itakapofika Julai Mosi dau lake litashuka na kufikia Pauni 105 milioni ambapo Barcelona italipa kupata saini yake.

Barcelona inahitaji kuzichanga Pauni 250 milioni kutoka kwenye mauzo ya wachezaji wake na ndio maana inadaiwa kwamba kuna wachezaji wasiopungua 10 wataonyeshwa mlango wa kutokea kwenye dirisha lijalo la usajili.

Kwenye orodha hiyo ya wachezaji wanaotajwa huenda wakauzwa yupo staa wa Kibrazili, Philippe Coutinho, huku mastaa wengine ni Samuel Umtiti, Ivan Rakitic, Malcom, Jasper Cillessen, Andre Gomes, Denis Suarez, Rafinha na Nelson Semedo.