Zlatan kumalizaka soka lake Hammarby

Muktasari:

Amecheza ligi zote kubwa barani Ulaya na kubeba mataji kibao na sasa anarejea nyumbani ambako, inaaminika atamalizia soka lake.

SAA chacha baada ya Kocha wa Tottenham Hotspurs, Jose Mourinho kueleza kwamba hana mpango wa kumrejesha kwenye soka la England, Zlatan Ibrahimovic, amefichua mahali ambako anakwenda kumalizia soka lake.

Ibrahimovic, ambaye amecheza kwa mafanikio klabu za Inter Milan, AC Milan, Barcelona, Man United, Ajax na  PSG kabla ya kutimkia zake Marekani akikipiga LA Galaxy, amefichua kuwa anakwenda kukipiga klabu ya Hammarby ya Ligi Kuu ya Sweden.

Mapema leo Zlatan alipoti kwenye kurasa zake za mitandao ya kijamii jezi ikiwa na jina lake nyuma kama alivyofanya wakati akijiandaa kutua Manchester United.

Zlatan aliweka jezi ya Hammarby ikiwa na jina lake nyumba na baadaye akaweka upande wa mbele kisha akaandika maneno kuashiria kuwa anatua Sweden.

Mourinho amekuwa shabiki mkubwa wa Zlatan tangu akiwa Barcelona na baadaye akiinoa Man United akamchukua mkongwe huyo kumfanyia kazi ya kufunga mabao.

Ibrahimovic (38) ameachana na LA Galaxy baada ya kumaliza mkataba wake wa miaka miwili ya kuwatumikia wababe hao wa MSL, aliojiunga nao kama mchezaji huru akitokea Old Trafford ambako pia alimaliza mkataba wake wa mwaka mmoja.

Hata hivyo, baadhi ya klabu ikiwemo Inter Milan, AC Milan, Juventus, Napoli na Bologna zilikuwa kwenye mchakato wa kuzungumza na Zlatan ili kunasa huduma yake.